Yanga: Hatujui sababu za kutoalikwa mkutano wa CAF

UONGOZI wa Yanga umetoa kauli juu ya kutoalikwa katika Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), bado hawajajua sababu za kutopewa mualiko.

Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Yanga wakili Simon Patrick akizungumza na kituo cha radio cha E-fm amesema wamelazimika kufuatilia mkutano huo kupitia mitandao baada ya kutopata mualiko.

Simon amesema Yanga ambao ni mabingwa wa nchi walitamani kuwepo katika mkutano huo unaonendelea jijini Arusha na kuhudhuriwa na Rais wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).

"Bahati mbaya hatujajua kipi kimetokea na sisi (Yanga) kukosa mualiko, tuliamua kutumia fursa ya teknolojia tuweze kufuatilia mkutano huu,"amesema Simon.

"Ni jambo jema tunafurahi limerfanyika hapa Tanzania, kwa manufaa mapana ya nchi yetu wamepata kutangaza utalii, wamepata kujionea mazuri ya Tanzania."

Aidha Simon ameongeza ingawa mkutano huo ni wa CAF lakini wanafahamu kwamba Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ndio walipaswa kutambua nafasi ya Yanga kushiriki mkutano huo kwa kuwapa klabu yao mualiko.