Ofisi ya Afisa Madini Mkazi Mirerani inavyorahisisha shughuli za uchimbaji

Ofisi ya Afisa Madini Mka­zi (RMO) Mirerani inayo­hudumia Wilaya ya Siman­jiro inafanya shughuli zake ambapo madini yanayopa­tikana ni Tanzanite, Graph­ite, Marble, Green Garnet, Ruby, Rhodolite, Tourma­line, Limestone, Magnesite na Feldspar.

Afisa Madini Mkazi (RMO) wa Mkoa wa kimadini wa Mirerani, Mhandisi Menard Msengi anasema ofisi yake ina jumla ya wafanyakazi 28 wa kudumu wa kada za uhandisi migodi, jiolojia, mazingira, jiomolojia, mifu­mo ya kompyuta, umeme, uhasibu na watumishi saba ambao ni wa mikataba ambao kazi zao kuu ni wak­aguzi wasaidizi wa madini.

RMO Msengi anasema shughuli za uchimbaji kwe­nye ukuta zinaongozwa na kanuni maalum na zinazo­simamiwa na kamati tend­aji ya eneo tengefu la ukuta (MCA) ambalo lina wajumbe wa taasisi mbalimbali na Mwenyekiti wake ni Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro na Katibu ni afisa madini mka­zi.

Amewataja wajumbe wa kamati hiyo ni taasisi za jeshi la polisi, ofisi ya usal­ama wa Taifa, uhamiaji, Takukuru, ofisa tarafa, ofisa mtendaji mkuu wa mamlaka ya mji mdogo wa Mirerani, mwakilishi wa chama cha wachimbaji madini Mkoa wa Manyara (Marema) Tawi la Mirerani na viongozi wa vijiji vinavyozunguka eneo la machimbo.

RMO Msengi anasema ofisi hiyo imefanikisha makusanyo ya Sh 2.6 bil­ioni kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023 sawa na asil­imia 52.23 ya malengo wali­yowekewa.

Ametaja baadhi ya saba­bu zilizochangia wasifikie malengo ni shughuli za kiji­olojia mashapo kuwa katika kina kirefu hivyo migodi mingi kutumia muda mrefu kufanya utanuzi na uwekez­aji mdogo.

“Pia ukosefu wa teknolo­jia za kisasa kwa wachim­baji wadogo, mvua ziliathiri miundombinu ya uchimbaji na usafirishaji madini ujen­zi, ukosefu wa miundom­binu ya umeme kwenye baa­dhi ya machimbo ya vito,” anasema RMO Mhandisi Msengi.

Anataja mikakati waliyo­nayo ni kuongeza vituo vya madini ujenzi, kulingana na jiografia ya Wilaya ya Siman­jiro, utoaji wa elimu kwa wafanyabiashara wa madi­ni wasio rasmi ili waweze kukata leseni, kufuatilia na kusimamia kwa kina miradi ya ujenzi wa viwanda vya madini ya kinywe.

“Pia tunaendelea kutoa elimu zaidi kwa wachimbaji ili kuweza kupunguza ajali kwenye shughuli za uchim­baji wa madini,” anasema RMO Mhandisi Msengi.

Anasema soko la madini linaendelea vizuri na kuna wafanyabiashara wakubwa (Dealers) 27 mpaka sasa na pia ujenzi wa soko lita­kalotumika kuwahudumia wafanyabiasha wa madini ya Tanzanite unaendelea chini ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).

Anasema kazi za uchimba­ji madini zinazofanyika kati­ka eneo tengefu la machim­bo ya madini ya Tanzanite, lina ulinzi wa kutosha muda wote ambapo pia kuna taa na kamera zinazofanya kazi muda wa saa 24.

“Eneo la machimbo ya madini ya Tanzanite limegawanyika katika vitalu mbalimbali ikiwemo kitalu A na C ambalo ni eneo la wachimbaji wakubwa na kitalu B na D ni eneo la wachimbaji wadogo,” anas­ema RMO Mhandisi Msengi.

Anasema eneo la kitalu C, linalomilikiwa na mwekez­aji kampuni ya Franone Mining and Gems LTD, lin­aendelea vyema na shughuli za uchimbaji madini.

Anasema udhibiti wa madini kwenye machimbo ya Tanzanite huanzia migo­dini chini ambapo kunaku­wa na wadhibiti wa madini wa Serikali na wadhibiti wa mwenye mgodi, wadhibiti wa mwekezaji na wachim­baji wenyewe.

“Madini hukusanywa na kuwekwa kwenye mfuko na baadaye hufungwa lakiri ya Serikali pamoja na ya mwe­nye mgodi kisha hupandish­wa juu,” anasema RMO Mhandisi Msengi.

Anasema madini yanapo­fika juu hupokelewa na afisa wa Tume ya Madini aki­shuhudiwa na maofisa wa vyombo vyote vya usalama na mamlaka ya mapato nchi­ ni (TRA), madini hupimwa na kurekodiwa na baadaye hufungwa tena lakiri.

“Baada ya hapo madini hayo huletwa kwenye jen­go la kituo cha Tanzanite Magufuli kwa ajili ya kufany­iwa uthaminishaji unao­fanywa ana maofisa wata­alamu wa ofisi ya madini wakishuhudiwa na vyombo vyote vya usalama,” anas­ema RMO Mhandisi Msengi.

Anasema baada ya hapo mteja hulipa stahiki za Seri­kali na baadaye hupewa kibali cha kupeleka madi­ni hayo sokoni na sokoni madini hupokelewa na afisa wa Tume ya Madini na kurekodiwa na baadaye mteja huruhusiwa kuuza madini yake kwa wafanya­biashara wakubwa walipo sokoni (Dealers).

“Shughuli zote za madini zinamalizika soko la madini ambapo pale kuna wafanya­biashara wakubwa wa madi­ni (Dealers), wachimbaji na wafanyabiashara wa kati (brokers) hufanya biashara zao za kuuza madini hayo na Dealers husafirisha madini hayo nje ya nchi baada ya kupata vibali husika,” anas­ema RMO Mhandisi Msengi.

Anasema kwa sasa chan­gamoto mbalimbali zilizopo kwenye maeneo ya machim­bo ni pamoja na ukosefu wa huduma za kijamii, maji safi na salama, umeme, mawasiliano na huduma za afya.

Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar atem­belea ujenzi wa soko la madini

Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mgeni Hassan Juma ame­tembelea soko la madini ya Tanzanite linalojengwa mji mdogo wa Mirerani wilay­ani Simanjiro mkoani Man­yara na kusema kuwa lita­zidi kuitangaza Tanzania na kuvutia watalii zaidi.

Mgeni ameyasema hayo baada ya kutembelea soko la madini ya Tanzanite lin­alojengwa mji mdogo wa Mirerani, akiwa na Mawazi­ri watatu na manaibu mawa­ziri watano na wajumbe wa Baraza la wawakilishi Zan­zibar.

Anasema ujenzi wa soko hilo utaitangaza zaidi Tanzania kupitia madini ya Tanzanite kwani wale waliokuwa na dhana potofu kuwa madini hayo yanapa­tikana nje ya Tanzania wataelewa.

“Tumeambiwa Tanzanite ni madini pekee duniani yanayopatikana Tanzania hivyo soko hilo la madini hayo litakapokamilika hapa Mirerani litaongeza sifa ya nchi na zaidi kuitangaza Tanzania kimataifa," anas­ema Mgeni.

Mkuu wa Mkoa wa Man­yara, Queen Sendiga anas­ema ujenzi wa soko hilo umefikia asilmia 65 ili jengo likamilike na wanatarajia hadi mwezi Oktoba mwaka 2023 litamalizika.

"Tunatarajia jengo la soko la madini kukamilika kwenye kilele cha mbio za mwenge wa uhuru ambao kwa mwaka huu 2023 zita­hitimishwa hapa kwetu Mkoani Manyara," anasema Sendiga.

Pia, ameishuku Serikali ya awamu ya sita inayoon­gozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa namna ina­vyofanikisha miradi mingi mikubwa na midogo mkoani Manyara.

Mhandisi wa ujenzi wa soko hilo la madini Goodluck Masika anasema walianza shughuli za ujenzi Mei 22 mwaka 2022 na wanatarajia kukamilisha mwezi Oktoba mwaka 2023.

Mhandisi Masika anas­ema mradi wa soko hilo unatekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa thamani ya Sh5.49 bilioni chini ya mshauri chuo cha ufundi Arusha.

Afisa madini mkazi (RMO) Mirerani, Mhandisi Menard Msengi anasema kukamilika kwa soko hilo kutaongeza tija kwenye mnyororo wa thamani ya madini ya Tan­zanite.

“Soko la madini ya Tan­zanite linaendelea vyema hiyvo likikamilika litaan­za kazi mara moja kwani tunatekeleza agizo la Seri­kali la kuwepo na soko la madini ya Tanzanite mahali madini haya yanapochimb­wa,” anasema Mhandisi Msengi.

Julai 7 mwaka 2021, Wazi­ri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa mji mdogo wa Mire­rani, aliagiza kwa kutoa miezi mitatu, shughuli za uuzaji na uongezaji thamani wa madini ya Tanzanite zifanyike Mirerani na soko lijengwe.