Zawa yapiga hatua katika upatikanaji wa maji

Muktasari:

Katika kuhakikisha hali ya upatikanaji wa maji safi na salama inakuwa nzuri, Zawa chini ya usimamizi wa Serikali kuu iko katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji. Miongoni mwa miradi hiyo ni pamoja na mradi wa uchimbaji visima unaofadhiliwa na Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China, mradi wa maji safi na usafi wa mazingira wa Mkoa wa Mjini Magharibi–ADF 12, mradi wa kuimarisha miundombinu ya maji ya mkoa wa Mjini-JICA.

Kiwango cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya taifa lolote kinapimwa na uwepo wa maji ya kutosha na yenye ubora unaohitajika. Zanzibar ikiwa ni nchi inayopambana kufikia Mapinduzi ya kiuchumi imebarikiwa kuwa na vyanzo mbalimbali vya maji vinavyosaidia ukuzaji wa uchumi wa taifa.

Licha ya uwepo wa rasilimali hii muhimu kama haitasimamiwa vyema bado haitatukwamua kimaendeleo.

Jukumu la kuhakikisha upa-tikanaji wa maji safi na salama pamoja na kulinda na kuhifadhi rasilimali za maji kwa Zanzibar liko chini ya Mamlaka ya Maji Zanzibar (Zawa) iliyoanzishwa chini ya Sheria ya Maji, Namba 4 ya Mwaka 2006.

Katika kuhakikisha hali ya upatikanaji wa maji safi na salama inakuwa nzuri, Zawa chini ya usimamizi wa Serikali kuu iko katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji. Miongoni mwa miradi hiyo ni pamoja na mradi wa uchimbaji visima unaofadhiliwa na Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China, mradi wa maji safi na usafi wa mazingira wa Mkoa wa Mjini Magharibi–ADF 12, mradi wa kuimarisha miundombinu ya maji ya mkoa wa Mjini-JICA.

Mradi wa uhuishaji na uimar-ishaji wa mfumo wa usamba-zaji maji Zanzibar – Exim Bank India, mradi wa utekelezaji wa uchimbaji wa visima vya Ras Al Khaimah ambapo hatua mbalimbali za uendeshaji wa visima hivyo kwa kazi za upelekaji umeme, ujenzi wa vibanda vya kuendeshea pampu na ulazaji mabomba makubwa na madogo kwa juhudi za Seri-kali kupitia Mamlaka ya Maji Zanzibar (Zawa) zimeanza na zinaendelea vizuri.

Lengo kuu la miradi hiyo ni kuendelea na usambazaji wa huduma ya maji safi na salama kutoka asilimia 87 mwaka 2015 hadi asilimia 97 mwaka 2020 mijini na kutoka asilimia 70 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 85 mwaka 2020 vijijini ambapo kazi mbalimbali hufanyika ikiwemo ulazaji wa mabomba, uwekaji wa pampu na mota mpya, ujenzi wa vibanda vya kuendeshea pampu, ujenzi wa matangi ya kuhifadhia maji, ujenzi wa ofisi za wilaya ya Kusini na ofisi za Magharibi “A” uchimbaji/uhuishaji wa visima vya maji.

Moja ya mradi mkubwa ambao kukamilika kwake unaweza kuwa ni ufumbuzi mkubwa wa huduma hiyo visiwani hapa, ni mradi wa usambazaji wa maji mjini ambao unakadiriwa kugharimu zaidi ya dola za kimarekani milioni 21, ambao unaendeshwa chini ya usimamizi mkuu wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (Zawa) pamoja na China.

Meneja wa mradi huo, Maulid Hassan Khamis alisema mradi huo unahusisha ukarabati na uchimbaji wa visima, ambapo visima 23 vimekarabatiwa na kuwekewa mitambo mikubwa ya kusukumia maji, na visima sita vipya vimechimbwa na kuweka mitambo mikubwa ya kusuku-mia maji kwa wananchi.

Alisema eneo jingine la mradi huo ni ujenzi wa matangi mawili makubwa ya kuhifadhia maji na usambazaji na mabomba, ambapo tangi moja lipo Saateni Mjini Unguja ambalo lina uwezo wa kuchukua lita milioni mbili za maji na tangi jingine lililopo Kilimani Mnara wa Mbao lina uwezo kuchukua lita milioni moja za maji.

Alisema mradi huo ulioanza mwaka 2013 na ambao tayari umekamilika rasmi na kuzinduliwa na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein hivi karibuni, utakuwa ukizalisha lita milioni 36.7 za maji ikiwa ni ongezeko kubwa la maji ukilinganisha na lita milioni 17 zinazozalishwa hivi sasa.

Udhibiti wa maji

Mamlaka ya Maji Zawa katika katika kuhakikisha suala la udhibiti wa maji linafanikiwa wamekuja na mradi wa ufungaji wa mita za maji katika maeneo mbalimbali.

 Alisema mradi huu wenye lengo la kutatua kero ya ukosefu wa maji safi na salama katika Mkoa wa Mjini Magharibi, hususan maeneo ya Mji Mkongwe na Ng’ambo ya Asili, unaogharamiwa na kutekelezwa kwa pamoja kati ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kwa jumla ya milioni 15.6, sawa na USD milioni 23.673. Mradi huu una vipengele vikuu vitatu ambavyo ni:- Uimarishaji wa miundombinu ya maji, ujenzi wa vyoo na usafi wa mazingira, kuijengea uwezo Zawa. Kwa upande wa ufungaji wa mita, Mamlaka ya Maji Zanzibar (Zawa) imeweza kufunga jumla ya mita 3,706 kwa upande wa Unguja na mita 1,446 kwa upande wa Pemba ambapo kazi hiyo kwa sasa itakuwa ni endelevu.

Mambo mengine yanayofanywa katika udhibiti wa maji ni kuendeleza jitihada za kuhuisha miundombinu ya maji ili kupunguza upotevu wa maji, kuhifadhi, kutunza na kulinda vyanzo vya maji pamoja na maeneo ya hifadhi ya maji.