Profesa Kitila: Lowassa kubali yaishe

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Kitila Mkumbo. PICHA|MAKTABA

Muktasari:

Alisema licha ya mchuano mkali kati yake na mgombea wa CCM anatakiwa kukubali matokeo.

Dar es Salaam. Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Kitila Mkumbo amesema aliyekuwa mgombea wa urais wa Chadema, Edward Lowassa, hana budi kukubali matokeo licha ya kupoteza nafasi hiyo. 

Pia Profesa Mkumbo alisema mgombea huyo kisheria, hakuwa na haki ya kujitangaza mshindi wa nafasi ya urais katika uchaguzi wa mwaka huu.

Juzi, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilitangaza matokeo ya kura za urais zilipopingwa Jumapili, Oktoba 25 mwaka huu na kumtangaza mgombea wa urais kwa tiketi ya CCM, Dk John Magufuli mshindi, lakini Lowassa siku hiyo pia alisema ameshinda katika uchaguzi kwa kura 10,268,795 sawa na asilimia 62 na kuitaka tume hiyo kumtangaza mshindi.

Profesa Mkumbo ambaye pia alipendekezwa na chama cha ACT- Wazalendo kugombea  nafasi hiyo na kukataa, alisema Lowassa aliingia kwenye kinyang’anyoro hicho akifahamu kuwa tume ndiyo yenye mamlaka ya kumtangaza mshindi.

Alisema licha ya mchuano mkali kati yake na mgombea wa CCM anatakiwa kukubali matokeo.

 “Hivyo Lowassa na  wenzake wa Ukawa hawana msingi wowote wa kisheria au kisiasa kutangaza ushindi wenyewe. Walikubali  kushiriki katika uchaguzi huu wakati wakifahamu kikamilifu kuwa NEC ndiyo yenye  jukumu la  kutangaza mshindi na mshindwa katika uchaguzi.”

Aliongeza: “Zaidi ya hayo, takwimu za uchaguzi zinaeleza pia.”

Hata hivyo alisema katika uchaguzi huu ambao ni wa kihistoria kutokana na upinzania mkali kati ya CCM na upinzani tofauti na miaka ya nyuma, bado upinzani umepoteza nafasi ya ubunge licha ya kujinyakulia viti 76 huku  CCM ikiwa na viti 188.

“Kupoteza viti hivyo ni ishara kwamba ushindi wa Lowassa haukuwa wa uhakika,”alisema Profesa Mkumbo na kuongeza;

“...nawashauri Ukawa kukubali kwamba Dk Magufuli ndiye rais mtaule wa awamu ya tano. Wahakikishe wanashirikiana  na kufanya kazi naye kazi kwa karibu katika kipindi chake cha miaka mitano ya uongozi. Kwa namna hiyo wataweza kuwa chachu ya kupata Katiba Mpya itakayowezesha kubadili mazingira ya kikatiba na kisheria katika uchaguzi ujao.”