Kwa nini tusiwapoteze wanaotaka kutupoteza?

Japo walijulikana, watu wasiojulikana walijulikana kwa unyama na ushenzi wao enzi zile za ubabe na uungu ngurumbili. Kuna mafyatu walipotezwa na mafyatu wasiojulikana bila hata kujulikana walikomaliziwa hadi sasa.

Taratibu, wasiojulikana wanaanza kujitangaza na kujulikana. Juzijuzi alijitokeza Fyatu asiyejulikana na akajijulisha kiasi cha kujulikana kuwa kumbe ni mmoja wa wale wasiojulikana. Huyu si mwingine, bali m/chair wa Umoja wa vitegemezi wa Chama cha Mafyatu UvCcM) kwa akina Nshomile aitwaye Fara S Baruhani aliyekaririwa akisema eti ndata wasiwatafute vijana ‘wanaomtukana’ mpendwa mtukufu Rahis kama wasiojulikana watawapoteza.

Ukimuona sura yake unaona anavyofanana na jina lake. Hivi hawajui hawa wanaotaka kupotezwa nao wana nguvu ya kuwapoteza wanaotaka kuwapoteza tena kwa kipande cha karatasi.

Asiyejulikana, kibwegeebwegee, alikaririwa akisema ndata “hawa tukiwapoteza msiwatafute. Piga makofi kwa CcM.” Bila aibu, waliokuwa wamehudhuria upupu huu walipiga makofi badala ya kumzaba makofi huyu asiyejulikana.

Bahati yake. Ningekuwapo, kingeumana kulaleki! Liwalo na liwe. Aliendelea kupokoma na kunyaaa…kwa mdomo, sorry, kupayuka. “Hivi wewe unajua gharama ya kumpata kiongozi?” Dashi! Halijui viongozi hata wasanii wanapatikana kwa kodi zetu.

Kuonyesha ubomu na uzwazwa alijifanya kuongelea maadili wakati ukiona uso wake ni madili matupu tena yanayofanyika kichawa na kichovu. Lazima mafyatu tuseme waziwazi, hatukubali kupotezwa. Heri wanaotaka kutupoteza wapotee, wapotezwe, hata wapotezane wenyewe kutokana na kutunyonya baada ya kujigeuza machawa.

Kama kupoteza ingekuwa inaruhusiwa kisheria, wa kupotezwa na kutokomezwa kwanza wangekuwa machawa maana wamezidi. Kila linaloamka na kukurupuka linajifanya linampenda rahis na kumtetea. Kwani, hana vyombo vya kunusanusa?

Je, huu ni usongo au laana? Liko wapi lile chawa lililotishia kuwataja wanaomtukana rahis bila kueleza wanamtukanaje wakati lenyewe ndilo kiongozi wa kumtukana kwa kutaka kumzidi kete?

Sijui inakuwaje. Tangu lini chawa wakawa na akili timamu zaidi ya mirija tu ya kunyonyea damu? Jamani, chawa, kunguni, na viroboto ni hatari kuliko nune ashibae na kunonea kwenye kinyesi cha wanyama. Heri nune hamdhuru yeyote zaidi ya kusaidia kutengeneza mbolea kuliko chawa mnyonya damu na mueneza magonjwa.

Jamani nifyatue lugha gani wahusika mnielewe? What kind of parlance do you want me to use for you to get it? Est que vous demandez que je parle Francais ou Chinois or Espanole? Naona yule anashangaa na mwingine kucheka. Mnadhani nabukanya au zwazwa na vihiyo kama hao chawa.

Mwenzenu ni daktari wa falsafa tena niliifyatulia ughaibuni; siyo madoktari wenu wanaojisifu walipata distinctions wakati wanaficha tasnifu zao. Ukitaka tasnifu yangu ya PhD nakupa. How fyatu fyatured Antestiopsis orbitalis Tanzanie chawalogists nd became the true defender of Fyatus globally.

Nirejee kwenye mada, kwa nini wahusika hawajiulizi ni kwa nini viongozi wanatukanwa, kama kweli wanatukanwa? Je, viongozi wanatukanwa au kuambwa ukweli? Je, kutukana siyo kudharau? Unategemea uheshimiwe wakati unafanya mambo ya aibu na ajabu kama kutishia kuwapoteza mafyatu? Je, wenye mtindio wa ubongo washindwao kutofautisha kutukana na kukosoa wanahitajika katika jamii ya mafyatu?

Nani apotee au kupotezwa kwanza, kama kupotezwa ni suluhu? Waliopotezwa wanatosha. Nashauri huyu fyatu anyakwe asitupotezee muda aeleze anavyopoteza mafyatu, anapowapoteza, kwa nini, kwa namna gani, na ameishapoteza wangapi hasa ambao hadi leo hatujui hata miili wala mabaki yao yalipo.

Hivi kuna tusi baya kama kumgeuza rahis mzima kuwa kama kichanga kisichoweza kujitetea au kujisemea hadi kutetewa na chawa? Rahis, namjua ni binadamu. Si chawa. Hata kama anaweza kufuga chawa asijue. Bado si chawa. Naamini hapendi chawa na machawa.

Je, yeye ndiyo anawafuga na kuwatuma hawa machawa waendelee kumchafua na kutuchefua wasijue mwakani tuna uchakachuaji au wameisha panga kuuchakachua? Washikeni adabu wasitutie vidole matoni tukawanyima kura za kula.

Naapa kwa jina la mababu, tutawaalanisha wapoteane na kupotezana wao kwa wao kabla ya kutupoteza mafyatu tusio na hatia, bali hatia moja tu kushindwa kuwafyatua hawa wasakatonge machawa, kunguni na viroboto mafyatu.

Acha nifyatue ushauri wa bure. Kama mmeishiwa sera, msemeni tuwapige tafu sisi madaktari wajuvi wa mambo. Kaya ni yetu sote kama alivyozoza doktri Nchimvi. Hatuombi nafasi japo tuna nafasi ya kuchangia ustawi wa kaya yetu badala ya kuichia vidudu vidogovidogo viinyevuenyevue na kuibunguabungua kana kwamba tu maiti.

Huyu fara, sorry Fara S Buriani ashindwe na kunyong’onyea au kupotelea mbali kwa jina la mababu zangu. Hii michawa mnaitoa wapi isiyosoma hata majira ya nyakati? Uchakachuaji uliopita mlichakachua na kupita kwa mbinde tena wakati ule akigombea madoadoa mwenzenu aliyewakimbia akaishia kuwarudia. Je, huu ujao mkipambana na fyatu kama mimi si kitakuwa kimbembe?

Pamoja na kujua hayo, bado mnaruhusu miduwanzi na midudu kutuchefua. Heri muipoteze hii kabla hatujawapoteza kwa njia ya kura ya kula yenu. Fyatu huwa hasemi bali mafyatu. Hivyo, msipuuzie madini haya.

Hivi leo ni siku gani na mwaka gani vile? Ngoja niwahi mafyatu wenzangu wasije wakajifatyua nikashindwa kuwafyatua.