Ben afunguka kinachokwamisha Bongo Movie, amtaja Kanumba

Muktasari:

  • Akizungumza na Mwananchi  Ben, amesema kuwa kwa sasa kwenye tasnia ya ugizaji kuna mabadiliko makubwa ambayo anakumbuka marehemu Steven Kanumba alikuwa akiyaota

Waswahili husema vya kurithi vinazidi, hivi ndivyo naweza kumuelezea mwigizaji wa Bongo Movie Abduli Ahmadi Salumu maarufu kama Ben au Serengo, ambaye amechukua mikoba ya uigizaji kutoka kwa babu yake marehemu mzee Pwagu ambaye alikuwa mwanzilishi wa kundi la sanaa Kaole.

Akizungumza na Mwananchi  Ben, amesema kuwa kwa sasa kwenye tasnia ya ugizaji kuna mabadiliko makubwa ambayo anakumbuka marehemu Steven Kanumba alikuwa akiyaota.

“Kitu kikubwa ambacho nakumbuka marehemu Kanumba aliwahi kukisema ili tasnia ya filamu ikue inatakiwa kuwe na mabadiliko kwa kuongeza wigo katika mataifa mbalimbali, kwa sababu kila siku alikuwa mtu wa kujaribu kitu kipya na alikuwa hakubali kushindwa.

"Hiyo ilimfanya marehemu kwenda nje ya nchi kufanya kazi na watu wengine na ndiyo kitu kinahitajika hata kwa sisi wasanii wengine kutoka kwenye mataifa mengine kwa ajili ya kuishindanisha sanaa,” amesema Ben.

Hata hivyo, ameeleza kuwa kwa sasa nguvu ya ushindani wa kwenda kufanya kazi na wasanii wa mataifa mengine kwenye upande wa uigizaji imepotea kwa sababu ya kutojiamini kwa baadhi ya wasanii.

“ Nguvu ya ushindani imepotea kwa sababu ya wasanii kutojiamini hasa wasanii wa kizazi hiki, unapokwenda kutengeneza kitu na wasanii wengine nje kinasaidia kujua mazingira tofauti, kupata pafomansi tofauti,” amesema Ben.

Pia ameeleza kuwa tasnia ya uigizaji ni kubwa na inaheshimika sana dunia, kama mtu akiitumia vizuri inaweza kumpa mafanikio makubwa na popote pale atatambulika.

“Tasnia ya uigizaji ni kubwa sana na duniani ina heshima kubwa na ndiyo maana Kanumba alikuwa na uthubutu wa kuweka wigo mkubwa ambao kwa wasanii wa sasa wanafurukuta na kufurukuta lakini bado kwa sababu tuna nidhamu ya uwoga,” anasema.

Hata hivyo, mwigizaji huyu ameenda mbali zaidi na kusema enzi hizo walibahatika kucheza filamu na watu wa nje ya nchi, wamejifunza mambo makubwa na ndiyo maana kwa upande wake hapati tabu kwani hakuna kitu kigeni na ndiyo maana akipewa uhusika wowote anautendea haki.

“Sisi tuliobahatika kucheza na wasanii kutoka nchi nyingine tumebahatika kuwa na madini makubwa na ndiyo maana mimi ukiniweka popote nanyoosha kwa sababu hata robo hatujawafikia wasanii wa nje,” amesema Ben.

Ben ameeleza kuwa kuna baadhi ya stori ambazo anafikiria angekuwa Kanumba angefanya vizuri zaidi kuliko zinavyofanywa na wasanii wengine.

“Kuna stori ambazo huwa nawaza ningekuwa na ile ‘mashine’ yangu Kanumba basi kila mtu angeacha kuangalia kwingine angetutazama sisi tu, lakini ndiyo hivyo hayupo tena,” amesema.

Mbali na hayo Beni amefunguka jinsi tasnia ya filamu ilivyompa mafanikio ambayo yanamsaidia kuendesha familia yake.

“Naweza nikasema bila filamu nisingefika hapa nilipo kwa sababu imenisaidia kutoka kuwa mlinzi hadi kuwa baba mwenye nyumba nikiwa na watoto wawili wa kike na wa kiume ambao wanasoma kwa kipato changu ninachokipata kupitia sanaa yangu,” amesema Ben.

Ikumbukwe kuwa kati ya filamu ambazo alifanya vizuri mwigizaji huyu ni Big Daddy, Village Pastor, Magic House, Pazia, na The Morning Alarm.