Makalla: Katiba si ya CCM wala Chadema, ni ya wananchi

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Amos Makalla

Muktasari:

  • Amos Makalla amesema suala la Katiba mpya ni la wananchi wote, si vyama vya siasa pekee.

Dar es Salaam. Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Amos Makalla amesema suala la kupatikana kwa Katiba mpya si la vyama vya siasa pekee bali la wananchi wote.

Kauli ya Makalla imekuja zikiwa zimepita siku mbili, tangu Makamu Mwenyekiti wa chama hicho (Bara), Abdulrahman Kinana alipozungumza na viongozi na maada wa chama hicho Mei 5, 2024 jijini Dodoma, kuhusu madai ya Chadema ya kutaka mchakato wa Katiba mpya uharakishwe.

Kinana aliyekuwa anajibu madai ya Chadema kuwa miongoni mwa mambo yaliyokwamisha mazungumzo ya maridhiano na CCM ni kutokubaliana kwenye muda na njia za kufanya mchakato wa Katiba.

Akizungumza katika mahojiano na waandishi na wahariri wa Mwananchi leo Mei 7, 2024 jijini hapa, Makalla amesema CCM imeshaweka wazi kuwa iko tayari kwa mchakato wa Katiba.

“Suala sio kusogeza mbele, suala ni tunalitekelezaje, tukubaliane. Hilo pia sio suala la vyama tu, Katiba lazima iende kwa wananchi. Hatutafanya Katiba ikawa ni ya CCM na Chadema, vyama vya siasa vina nafasi yake.

“Ni suala la muda, lakini haiwezekani kukawa na chama kimoja kikasema kinataka kesho, chama hakiko kimoja, kuna vyama vingi na wenyewe tupate maoni yao na mwisho wa yote kuna wananchi, taasisi, watu lazima katika hili mwende pamoja,” alisema.

Akizungumza na Mwananchi Jumapili Mei 5, 2024 Lissu alisema CCM imekuwa ikipiga danadana suala la Katiba mpya tangu mfumo wa vyama vingi uliporejeshwa mwaka 1992.

“Mwaka 1992 wakati Tume ya Jaji Francis Nyalali ilipotoa pendekezo la mabadiliko ya Katiba, CCM walisema iwe baada ya uchaguzi wa mwaka 1995 ukapita; ilipofika 2000, wakasema iwe 2005; ilipofika 2005 wakasema 2010.

“Rais Jakaya Kikwete (mstaafu) alipoleta Tume ya Mabadiliko ya Katiba mwaka 2012, ilipofika 2014 wakasema baada ya uchaguzi wa 2015,” alisema.

“Sasa Rais Samia naye kaingia anasema iwe baada ya uchaguzi wa 2025, nani mwenye akili atakayekubaliana nao?” alihoji.