Sheria ya Ununuzi yatajwa kuwa kichaka cha upigaji fedha za umma

Muktasari:

  • Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Dk Faraja Kristomus ameshauri kufanyiwa marekjebidho kwa Sheria ya Ununuzi inayoruhusu maofisa masuhuli wa Serikali kununua vifaa kwa zabuni na kjuongeza fedha za ucheleweshaji, jambo alilosema linachangia uchepushwaji wa fedha za umma.

Dar es Salaam. Upungufu uliomo katika Sheria ya Ununuzi umetajwa kuwa chanzo cha ubadhirifu wa fedha za umma, ambapo wadau wameshauri kufanya ununuzi kwa fedha tasilimu, huku pia wakiishauri Serikali kutathmini mfumo wa Force account kwani unaweza kuwa na udhibiti mkubwa wa fedha za umma.

Hayo yamesemwa na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Dk Faraja Kristomus leo Jumatano Novemba 8, 2023 wakati akifungua mada ya Mwananchi X Space inayosema “Nini kitarajiwe kuhusu ripoti ya CAG baada ya maazimio ya Bunge?”

“Sheria ya manunuzi ni moja serikalini bado hatujagatua mifumo ya manunuzi matokeo yake sasa tuna sheria moja, unaweza kukuta Chuo Kikuu cha UDSM idara yangu itahitaji kununua kitu lakini lazima kupelekwa kwenye zabuni.

 “Mnunuzi lazima ataongeza thamani ya bidhaa kwa kuwa anatarajia serikali itachelewa kumlipa fedha. Mfumo wa ununuzi utatoza milioni 9 au 8 kwa bidhaa ya milioni 2 sokoni wanaweka ziada kwa sababu mchakato wa kulipwa na serikali unachukua muda mrefu,” amesema.

Amesema hiyo imeifanya Serikali kubaki namadeni mengi kwa muda mrefu.

 “Tugatue mfumo wa manunuzi, taasisi isinunue kwa mfumo wa fedha iwepo fedha kwenye akaunti inunuliwe kwa bei ileile ya soko kwa mfumo huu tutaokoa fedha, tutaondoa uhusiano mbovu wa maofisa maduhuli, wanunuzi na wafanyabiashara wasio waaminifu,” amesema Kristomus.

Amesema miaka michache kabla ya kuelekea uchaguzi mkuu vitendo vya rushwa huwa ni vingi, “Natamani utafiti ufanyike katika eneo hili ili kubaini tabia za ubadhirifu Serikalini miaka michache kabla ya kuelekea uchaguzi.”

Amesema ana wasiwasi huenda matukio ya ubadhirifu yakawa ni makubwa na hofu ni kwamba nyuma ya ubadhirifu huo inawezekana kuna mikono isiyoonekana na ina uhusiano na chaguzi zijazo.

Kwa upande wake mhadhiri wa fedha, uhasibu na kodi wa Chuo Cha Serikali za Mitaa Dodoma, Charles Matekele amesema bado kuna maswali mengi ya kujiuliza baada ya kuona azimio la Bunge ikizingatiwa dosari zinazobainishwa na CAG ni zile zile.

“Mkaguzi anapofanya kazi yake huwa shirikishi kuanzia yule anayekaguliwa hadi kufikia kwenye jamii, hivyo ripoti anayotoa CAG inaposema fedha zimepigwa ni kweli zimepigwa na akisema ni uzembe basi kweli ni uzembe.

“Utalaam na weledi unazingatiwa sana kwenye ukaguzi hivyo wananchi waongeze imani kwa wakaguzi na wakaguliwa watimize wajibu wako,” amesema Matekele