Mashabiki Yanga washindwe wao tu

Dar es Salaam. Klabu ya Yanga kushirikiana na Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) wamezindua kadi za kimataifa za uanachama wa klabu hiyo inayofahamika kama ‘NBC Yanga Membership Card’. Hatua hiyo inatajwa kuwa pamoja na faida nyingine inalenga kurahisisha malipo ya uanachama kwa wanachama wa klabu hiyo na hivyo kusaidia kuongeza mapato ya klabu.

Hafla ya uzinduzi wa kadi hizo imefanyika hii leo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla fupi iliyohusisha viongozi waandamizi wa pande zote mbili, wafanyakazi benki hiyo, wanachama na mashabiki mashuhuri wa klabu ya Yanga. Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), Steven Mnguto alimuwakilisha Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia.

Katika kusaini makubaliano ya utekelezaji wa mpango huo, ilishuhudiwa Rais wa Klabu ya Yanga Mhandisi Hersi Saidi akiongoza zoezi hilo kwa niaba ya klabu hiyo huku upande wa benki ya NBC ukiongozwa na Mkurugenzi wa Biashara wa benki hiyo, Elvis Ndunguru aliemuwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi.

Akizungumza kwenye hafla hiyo Ndunguru alisema ikiwa kama mdhamini mkuu wa Ligi ya soka Tanzania (NBC Premier League), ligi Daraja la Kwanza (NBC Championship) na Ligi ya Vijana (NBC Youth League), benki hiyo imedhamiria kuonyesha kwa vitendo nia yake  ya kuleta mapinduzi halisi kwenye mchezo wa soka nchini kwa kuwekeza zaidi katika huduma mbalimbali zinazolenga kuboresha uendeshwaji wa vilabu vinavyoshiriki ligi hiyo ikiwemo suala zima la usajiri wa wanachama.

“Kadi hii tunayoizindua leo, imeambatana na faida nyingi ambazo wanachama wa Yanga watanufaika nazo ikiwemo urahisi wa kununua tiketi za mechi za timu yao za NBC Premier League, FA na CAF Champions League kwa mfumo wa N-Card. Wana Yanga sasa hawatahitaji tena kununua N-Card kwa kuwa kadi hizi tayari zimeunganishwa na mfumo wa N-Card. Kadi hii pia inaweza kutumika kufanya malipo katika vituo vyote vya TAMESA nchini ikiwemo malipo ya huduma ya Ferry -Kigamboni.’’

“Zaidi pia kupitia kadi hii wanachama wa Yanga watapata urahisi wa kutoa fedha kupitia mashine za fedha (ATMs) popote duniani, kufanya malipo bure kupitia mashine za malipo (POS) popote duniani, urahisi wa kufanya malipo ya mtandaoni yaani (online paymeu
nt) na urahisi wa kufanya malipo ya kidijitali kupitia mifumo ya NBC Kiganjani na Internet Banking.’’ Alifafanua.

Kwa mujibu wa Ndunguru, kadi hizo ambazo zina viwango vya kimataifa vya ulinzi na usalama, zitapatikana maeneo mbalimbali ikiwemo matawi yote 67 ya Benki ya NBC na mawakala wa benki hiyo zaidi ya 60,000 waliopo nchi nzima.

“Mbali na kuwapa Wanachama wa Yanga uwezo wa kifikia fedha zao masaa 24 ndani na nje ya nchi kwa kupitia mtandao mpana wa Benki ya NBC, kadi hii pia ina faida kadhaa ikiwemo uwezo wa kufanya malipo mbalimbali na mengineyo,  punguzo la bei ndani na nje ya nchi kupitia wadau wa biashara wa Benki ya NBC,  malipo ya kidigali yaani (tap and pay) ambayo ni huduma mpya nchini, usalama ulioboreshwa kupitia teknolojia ya 3D na kubwa kuliko yote kadi hii pia iataumika kama kadi ya uanachama wa klabu ya Yanga (Wananchi)’’ aliongeza.

Awali akizungumza kwenye hafla hiyo Mhandisi Hersi Saidi alisema klabu hiyo inajivunia kuingia makubaliano hayo na Benki bora ya NBC Tanzania na kwamba hatua hiyo itaisadia sana klabu hiyo katika kuwahudumia wanachama wake hususani kwenye usajili na kutoa kadi za Uanachama.

"Ukijiunga kuwa Mwanachama wa Yanga, kupitia Benki ya NBC utapata kadi ya Uanachama na hapo hapo utapata huduma za kibenki. Lakini kubwa zaidi kadi ya NBC imeunganishwa na huduma za N CARD hivyo Mwanachama wetu atapata huduma ya kuingia Uwanjani pamoja na huduma za Usafiri" alibainisha Mhandisi huyo.

"Niwaombe pia Benki ya NBC kutazama fursa nyingi zilizopo ndani ya Klabu yetu tuna wanachama ndani na nje ya nchi na tunaamini Yanga ndio klabu sahihi ya kufanya nayo kazi kwenye sekta ya michezo,’’ aliongeza