Prime
Bajaber ategua mtego Simba
KIUNGO mshambuliaji wa Simba, Mohammed Bajaber amekiri kuwa bado hajaonyesha hata nusu ya uwezo wake ndani ya klabu hiyo kutokana na majeraha yaliyokuwa yakimsumbua lakini anaamini bado ananafasi ya kufanya makubwa akiwa na Wekundu hao wa Msimbazi.
Bajaber amesema kurejea kwake kwenye kiwango kizuri akiwa na timu ya taifa ya Kenya ni ishara kwamba anaendelea kupata utimamu na yupo tayari kupigania nafasi yake ndani ya kikosi cha Simba.
“Nimepitia kipindi kigumu kutokana na majeraha lakini sikuwahi kupoteza imani. Kufunga mabao mawili na kutoa asisti moja nikiwa na timu ya taifa ni ishara kwamba ninaendelea kurejea kwenye kiwango changu. Nataka kufanya makubwa zaidi Simba na kuonyesha kile ambacho mashabiki hawajakiona bado kutoka kwangu,” amesema Bajaber.
Kauli hiyo imekuja siku chache baada ya nyota huyo kuwa mmoja wa wachezaji waliovutia zaidi katika kikosi cha Kenya kilichoifunga Lesotho mabao 4-0 katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa uliochezwa mwishoni mwa wiki. Katika ushindi huo, Bajaber alifunga mabao mawili na kutoa asisti moja, akionyesha kiwango bora ambacho kilimfanya kuwa nyota wa mchezo huo.
Kiwango hicho ni habari njema kwa Simba ambayo imekosa huduma ya mchezaji huyo kwa muda mrefu kutokana na majeraha ya nyama za paja aliyoyapata Januari 18, 2026 katika mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Mtibwa Sugar uliomalizika kwa sare ya bao 1-1.
Kocha wa Simba, Steve Barker amesema Bajaber ni mchezaji mwenye ubora mkubwa ambaye ameathiriwa zaidi na majeraha.
“Kila mtu ameona ubora wake akiwa fiti. Kilichomrudisha nyuma ni majeraha pekee. Tunaendelea kufuatilia maendeleo yake na tukimpata akiwa katika hali nzuri, atakuwa sehemu muhimu ya mipango yetu,” amesema Barker.
Kwa upande wake, kocha wa Kenya, Benni McCarthy, amesema kiwango alichokionyesha Bajaber dhidi ya Lesotho ni uthibitisho kwamba mchezaji huyo amerejea baada ya kipindi kigumu.