Takwimu za Ubamba zaichanganya FC Masar
Muktasari:
- Takwimu zake msimu huu, nyota huyo wa zamani wa Fountain Gate Princess alifunga mabao 17 na kutoa asisti nane katika mashindano ya ndani na kimataifa.
WINGA wa kimataifa, Hasnath Ubamba, ameendelea kuthibitisha ubora wake katika soka la wanawake nchini Misri baada ya kumaliza msimu wa 2025/26 akiwa miongoni mwa nyota walioibeba FC Masar.
Takwimu zake msimu huu, nyota huyo wa zamani wa Fountain Gate Princess alifunga mabao 17 na kutoa asisti nane katika mashindano ya ndani na kimataifa.
Kiwango hicho kimeifanya klabu hiyo kuanza mpango wa kumboreshea mkataba wake ili aweze kusalia kikosini hapo baada ya ule wa awali kutamatika Julai 2027.
Ubamba, ambaye huu ni msimu wake wa pili inaelezwa viongozi wa Masar wamepanga kumboreshea mkataba mpya huku pande zote mbili zikikaribia kufikia makubaliano na kilichobaki ni yeye kumwaga wino.
“Ni mchezaji ambaye anatazamwa na timu nyingi pale Misri kwa hiyo Masar wana wasiwasi kama hawatamboreshea na kumuongezea mkataba mapema huenda msimu ujao ukawa ngumu kumbakiza.” kilisema chanzo cha karibu
Ubamba alionyesha ubora mkubwa kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa wanawake ambapo alifunga mabao mawili na kutoa assist moja, akichangia kwa kiwango kikubwa safari ya timu hiyo kumaliza nafasi ya nne kwenye mashindano hayo.
Kwenye michuano hiyo alionyesha kiwango kikubwa na kupewa Tuzo ya Mchezaji bora wa mechi na kuingia kwenye kikosi bora cha mashindano hayo.
Kutokana na mchango huo, FC Masar imeonyesha nia ya kuendelea kuwa naye kwa kuandaa mkataba mpya wenye maboresho ya kimaslahi ili kuzuia klabu nyingine zinazomfuatilia kupata saini yake.