Mzee wa miaka 60 afia kwa mganga wa kienyeji akiongezewa nguvu za kiume

Muktasari:

  • Mzee alitokwa na damu nyingi na kuishiwa nguvu. 
  • Jeshi la polisi linamshikilia mganga huyo kwa tuhuma za kusababisha kifo cha mzee Joseph

Shinyanga. Mzee Joseph Sahn (60), mkazi wa Kijiji cha Nzonza wilayani Shinyanga amefia kwa mganga wa kienyeji Robert Mkoma mkazi wa kijiji hicho wakati akimpatia matibabu ya kumuongezea nguvu za kiume kwa kutumia pampu ya baiskeli.

Akizungumza ofisini kwake leo Jumatatu, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Simon Haule amesema tukio hilo lilitokea jana Jumapili saa 10:00 jioni nyumbani kwa mganga huyo, alipokuwa anamuwekea dawa ya unga kupitia tundu la uume wake kisha kuanza kuisukuma kwa kutumia pampu ya kujaza upepo kwenye baiskeli.

Kamanda Haule amesema wakati akipampu ili dawa hiyo iingie vizuri ndani, mzee huyo alianza kutokwa damu nyingi kwenye tundu hilo na kisha kuishiwa nguvu. 

“Kutokana na kutokwa damu nyingi ilisababisha kifo cha mzee huyo, ambapo tayari jeshi la polisi linamshikilia mganga huyo kwa tuhuma za kusababisha kifo cha mzee Joseph,” amesema Kamanda Haule

Amesema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani ili ajibu tuhuma zinazomkabili. 

Kamanda Haule aliwataka wananchi kuacha kuona waganga kuwa kimbilio la matatizo yao badala yake wakimbile hospitalini au kwenye vituo vya afya vilivyokaribu nao.