Mambo manane kutikisa kikao cha makinikia

Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati Maalumu iliyoundwa na Rais John Magufuli kufanya mazungumzo na ujumbe wa Barrick Gold Corporation kuhusu biashara ya madini yanayochimbwa na migodi ya kampuni hiyo nchini akiwa na wajumbe wa kampuni hiyo kabla ya kuanza kwa mazungumzo hayo Ikulu jijini Dar es Salaam juzi. Picha na Ikulu

Muktasari:

Mazungumzo kati ya Serikali na kampuni ya Barrick Gold yameanza huku Watanzania wakisubiri kwa hamu kujua hatima yake.

Dar es Salaam. Baada ya siku 160 tangu usafirishaji wa mchanga wa madini ulipozuiwa na baadaye kuundwa kwa kamati mbili na Rais John Magufuli kuchunguza biashara hiyo nchini, hatimaye mazungumzo kati ya pande mbili yameanza.

Mazungumzo kati ya Serikali na kampuni ya Barrick Gold yameanza huku Watanzania wakisubiri kwa hamu kujua hatima yake.

Licha ya kwamba hakuna upande ambao umesema kitakachojadiliwa, kuna hoja muhimu nane ambazo zinaweza kuibuka na kuchukua nafasi kubwa katika mazungumzo hayo.

Ripoti za kamati

Tangu ripoti zote mbili zilipowasilishwa kwa Rais mwishoni mwa Mei na mwanzoni mwa Juni, taarifa zake zilipingwa na Acacia ambayo ilienda mbali zaidi na kusema haikupewa nakala kuona kilichomo.

Madai yote yaliyobainishwa ikiwamo kiwango kikubwa na aina nyingi za madini yaliyomo kwenye makinikia kwenye makontena 277 yaliyozuiliwa Bandari ya Dar es Salaam pamoja na kodi inayokadiriwa kufika Sh108 trilioni, yalipingwa na kampuni hiyo iliyosisitiza kwamba wakati wote imekuwa ikitoa taarifa sahihi.

Acacia ilifika mbali na kusema endapo ingekuwa inafanya udanganyifu wa kiwango na wingi wa madini ndani ya makinikia kama ilivyoripotiwa na kamati za Rais, basi migodi yake miwili ingeongoza kwa uzalishaji wa dhahabu duniani.

Mkaguzi huru

Kutokana na kutoridhishwa na ripoti za kamati, Acacia ilisisitiza kuhitaji kuundwa kwa tume huru ya uchunguzi kuhusu suala hilo jambo ambalo halikuungwa mkono na Serikali. Pia, Rais Magufuli alitoa msimamo akiwa kwenye ziara ya kikazi kanda ya magharibi kwamba endapo kampuni hiyo itachelewa kuja kufanya mazungumzo, atafuta leseni yake.

Wengi wanaamini kuwa suala la mkaguzi huru litachukua nafasi katika majadiliano hayo wakati timu za watalaamu wa Tanzania na wale wa kampuni ya Barrick Gold wanapotafuta ufumbuzi wa mgogoro huo.

Kodi ya Sh424 trilioni

Hivi karibuni, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilikadiria kiasi cha Dola 40 bilioni za Marekani (zaidi ya Sh89 trilioni) ikiwa ni kodi iliyokwepwa pamoja na faini na riba yake, Dola 150 bilioni (zaidi ya Sh335 trilioni).

Kutokana na utata uliopo hapa, kipengele hicho nacho kinatarajiwa kuwa na mvutano kabla muafaka haujapatikana. Wapo waliosema malipo ya Sh424 trilioni kutokana na ukokotozi wa TRA hayawezekani, lakini endapo itakuwa kinyume chake, Tanzania itakuwa nchi ya kipato cha kati.

Usafirishaji makinikia

Hili ni suala nyeti lililosababisha kutumbuliwa kwa aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Profesa Justin Ntalikwa, mabadiliko ya sheria ya madini iliyopunguza madaraka ya waziri kwenye eneo hilo, kuvunjwa kwa Bodi ya Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) na kuanzishwa kwa kamisheni ya madini.

Kuhakikisha suala hili linakuwa endelevu, Serikali imeagiza kujengwa kwa mtambo wa kuchenjulia mchanga huo nchini. Hoja kadhaa za kupinga uwezekano huo ziliibuliwa na wadau, lakini Serikali imeendelea na msimamo huo na kukazia imeliweka kwenye sheria mpya.

Acacia yenyewe inasema mkataba unairuhusu kufanya hivyo na kuuza mchanga huo popote duniani ambako mteja atapatikana. Serikali ikishinda kipengele hiki huenda ombi la Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche kwamba mtambo huo ujengwe inakochimbwa dhahabu litatimia.

Mikataba ya madini

Kwenye Bunge la Bajeti lililomalizika hivi karibuni, Serikali iliwasilisha kwa hati ya dharura miswada miwili ya sheria mpya za rasilimali. Serikali pia iliwasilisha mswada wa mabadiliko ya sheria mbalimbali ikiwemo Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 ambayo yaliigusa mikataba ya utafutaji, uchimbaji na biashara ya sekta hiyo kwa ujumla.

Miongoni mwa matakwa yaliyomo kwenye sheria hizo mpya ni kuwapo kwa majadiliano kwenye mikataba iliyopo ili kuondoa vipengele vyote vinavyoinyonya Serikali na kuwanufaisha wachimbaji.

Licha ya sheria hizo mpya zilioweka asilimia moja ya ada ya ukaguzi kwa madini yanayosafirishwa kwenda nje ya nchi, Sheria ya Fedha ya mwaka 2017 imeongeza mrabaha kwa asilimia moja kutoka nne zilizokuwapo kwenye mikataba mingi ya madini inayotumika hivi sasa. Sheria hizo mpya pia zimeleta mabadiliko makubwa ambapo sasa wawekezaji hawataruhusiwa kupeleka malalamiko yao yanayoruhusu rasilimali za Tanzania nje ya nchi kwenye mahakama za usuluhishi wa migogoro ya biashara za kimataifa. Wakati hayo yakitokea, tayari Acacia imekwenda kwa msuluhishi wa kimataifa kama inavyoelekezwa na mikataba ya madini kati ya mwekezaji na Serikali. Hili nalo huenda likachukua nafasi kubwa katika mazungumzo yanayoendelea.

Mikataba ya kimataifa

Miongoni mwa mambo yaliyoibua mjadala mkubwa bungeni wakati wa kujadili miswada mitatu ya mabadiliko ya sheria ya madini ni hatua zilizochukuliwa na Serikali kuzuia makontena 277 ya kutosafirishwa nje ya nchi wakati mikataba inaruhusu hilo.

Waliotahadharisha walisema kilichofanywa ni kinyume na mikataba ya kimataifa ya uwekezaji ambayo Tanzania imeiridhia.

Suala hilo nalo linaweza kuwa sehemu ya majadiliano na endapo hakutakuwa na muafaka, shauri hilo linaweza kupelekwa kwenye mahakama za kimataifa za usuluhishi wa migogoro ambako tayari Acacia imefungua kesi ingawa ina matumaini makubwa kwamba suluhu itapatikana.

Masilahi ya pande zote

Ingawa Barrick na Acacia zipo kwenye mataifa mengi duniani ambako zinaendesha shughuli za utafiti na uchimbaji wa madini, kiasi kikubwa cha madini yake kwa sasa kinatoka nchini na kuifanya iwe kampuni kubwa ya usafirishaji wa dhahabu Afrika.

Kampuni hizo zitakuwa na wakati mgumu kufunga migodi yake nchini na ndio maana suala hilo la masilahi ya pande zote mbili linaweza kuchukua nafasi yake katika majadiliano hayo.

Ugumu huo unatokana na ukweli kwamba Acacia wakiondoka, watalazimika kuwa na kipindi cha mpito cha kutokuwa na bidhaa sokoni kutokana na kutokuwa na uzalishaji sehemmu nyingine yoyote duniani, ingawa inaendelea na utafiti kwenye mataifa kadhaa.

Lakini, muafaka ukipatikana utaiwezesha Tanzania kutimiza ndoto yake ya kukuza mapato yatokanayo na sekta ya madini hasa dhahabu, kujengwa kwa mtambo wa kuchenjua makinikia pamoja na maghala ya kuhifadhi madini bila kusahau Benki Kuu (BoT) kuanza kutunza dhahabu kama akiba za Serikali.

Nafasi ya Acacia

Kitakachokubaliwa katika majadiliano kati ya Barrick na Serikali kitapelekwa kwenye uongozi wa Acacia ambayo ina uamuzi wa ama kukubali au kukikataa.

Hata hivyo, Barrick ina hisa nyingi Acacia hivyo kuwa na nafasi kubwa ya kutoa uamuzi.

Maoni ya wadau

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPASF), Godfrey Simbeye alibainisha kutotambulishwa kwa timu ya wataalamu wanaoiwakilisha Serikali kwenye mazungumzo hayo na akasema huenda Serikali imewatafuta baadhi kutoka nje ya nchi.

Alisema pamoja na kitakachoamriwa kwenye majadiliano hayo Tanzania itakuwa na jukumu la kujisafisha kimataifa.

“Tanzania itakuwa na jukumu la kujisafisha kimataifa juu ya mazingira yake ya uwekezaji. Tumechafuka huko nje. Suala muhimu sio amani iliyopo, bali uhakika wa kuwa na uwekezaji endelevu ndiyo maana wawekezaji wanaenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo licha ya mapigano yanayoendelea.”

Akitambua umuhimu wa ripoti za kamati za Rais, alisema kama kilichobainishwa ni sahihi basi kuna haja ya kujiuliza kwa nini Serikali imewafikisha hapa Watanzania kwani ina kila kitu kuchunguza na kuzuia udanganyifu wa namna hiyo kutokea.

“Sheria inayotoa uhuru wa kupitiwa na kubadilishwa kwa mikataba ni mbaya zaidi kwa uwekezaji,” alitahadharisha.

Profesa Haji Semboja wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), alikuwa na mtazamo tofauti kidogo kuhusu faida za majadiliano hayo.

Alisema endapo tuhuma zilizopo zitamalizika dunia itaelewa zaidi.

“Acacia watapata heshima kwa uwezo wa kushughulikia migogoro inayoweza kujitokeza dhidi yake vivyo hivyo kwa serikali,” alisema msomi huyo.

Hata wakibainika walikwepa kodi kama kamati ilivyobainisha, alisema itahitaji kujichunguza kuhusu mifumo yake ya ndani. “Inawezekana ni watumishi wachache waliokuwa wanafanya hivyo,” alieleza Profesa Semboja.

Mbunge wa Kinondoni (CUF), Maulid Mtulia alisema busara kubwa itatumika kurekebisha kasoro zote zilizopo kabla ya kuupata muafaka.

“Wawekezaji wasiwe na wasiwasi wa kufutiwa mikataba yao itakapoanza kutekelezwa sheria mpya inayoagiza kufikishwa bungeni kwa makubaliano yoyote yaliyoridhiwa na Serikali kuhusu uvunaji wa rasilimali za taifa,” alisema.