Mbunge CCM aburuzwa mahakamani, apata dhamana

Muktasari:

  • Mbunge huyo ameshitakiwa kwa kosa la kujihusisha na vitendo vya rushwa

 

Biharamulo. Mbunge wa Kishapu (CCM) Suleiman Nchambi na wenzake 10 wamefikishwa katika mahakama ya wilaya ya Biharamulo mkoani Kagera wakishtakiwa kwa kosa la kujihusisha na vitendo vya rushwa.

Wakizungumza mahakamani  leo Jumatatu Agosti 6, 2018 waendesha mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru),  Dismas Muganyizi na Joseph Mulebya wamesema watuhumiwa hao walifanya  miamala ya rushwa kinyume na  kifungu cha 15 cha sheria namba 11 cha mwaka 2007 ya taasisi hiyo.

Amesema watuhumiwa hao kwa nyakati tofauti katika mgodi wa Stamigold ulioko wilayani Biharamulo kati ya Septemba 2015 hadi Oktoba 2016 walitenda kosa la kufanya miamala ya rushwa na kuvunja kifungu cha 15(1) (a&b) cha sheria namba 11 ya mwaka 2007 ya kupambana na kuzuia rushwa.

Mbele ya hakimu wa mahakama hiyo, Flora Ndale, Muganyizi  amewataja washtakiwa hao kuwa ni Clara Mwaikambo, Chacha Wambura, Christopher Mwinuka,  Sadick Kaswia, Fortunatus Rulemeja, Reginald Haule, Yasini  Mohammed, Fabian Ngelela , Felician Edward, Braithony Luchagula  na Nchambi.

Amesema Nchambi na Mohammed, Oktoba 2016 walifanya muamala wa rushwa na kumpatia Sh5 milioni mhasibu wa Stamigold co. Ltd ambaye ni Clara kama zawadi ya kupatikana malipo yao ya dola 170,945 za Marekani walizokuwa wakidai katika machimbo ya mgodi huo.

Washtakiwa hao wamekana mashtaka hayo na kuachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya dhamana ya kuwa na wadhamini wawili wenye hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya Sh10milioni, huku mmoja akiwa mtumishi wa umma.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Septemba 3, 2018 itakapotajwa tena.