TCRA yazipiga rungu kampuni za simu

Muktasari:

Sambamba na adhabu hiyo, TCRA pia imezitoza kampuni hizo faini ya Sh500 milioni kila moja kwa kosa la kuathiri na kuhatarisha usalama wa umma na jamii ya Watanzania kwa kusajili laini bila kufuata utaratibu.

Dar es Salaam. Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imezitoza faini kampuni zote za simu kwa kusajili laini bila vitambulisho na kutofuata utaratibu.

Kampuni zilizotozwa faini hiyo na kiwango kikiwa kwenye mabano ni Airtel (Sh1.08 bilioni), Smart (Sh1.3 bilioni), Vodacom (Sh945 milioni), Zantel (Sh105 milioni) na Halotel (Sh1.6 bilioni).

Mkurugenzi wa TCRA, Mhandisi James Kilaba amesema leo (Julai 14) kuwa hii si mara ya kwanza kwa watoa huduma hao kukiuka sheria.

Kiliba amesema kutokana na kurudia kosa hilo, TCRA imezitoza kampuni hizo faini ambazo Airtel imetozwa Sh542 milioni, Smart (Sh37 milioni), Tigo (Sh625 milioni), Zantel (Sh52 milioni) na Halotel (Sh822 milioni).

Pia, kampuni hizo zimetozwa Sh500 milioni kila moja kwa kosa la kuathiri na kuhatarisha usalama wa umma na jamii ya Watanzania kwa kusajili laini bila kufuata utaratibu.