Wenyeviti 20 wa vijiji wamkimbia Mbowe

Mbunge wa Hai ni Freeman Mbowe ambaye ni mwenyekiti wa Chadema na Kiongozi wa Kambi Rasmi za Upinzani Bungeni.


Muktasari:

Uamuzi wa wenyeviti hao ni muendelezo wa viongozi wa vyama vya upinzani, hasa Chadema kuvihama vyama vyao na kujiunga na CCM


Arusha. Wenyeviti 20 wa vijiji wa Chadema katika jimbo la Hai mkoani Kilimanjaro wamehamia CCM leo Alhamisi Septemba 6, 2018.

Mbunge wa Hai ni Freeman Mbowe ambaye ni mwenyekiti wa Chadema na Kiongozi wa Kambi Rasmi za Upinzani Bungeni.

Majina ya wenyeviti hao na vijiji vyao katika mabano ni, Hendry Kimaro (Lukani), Josephat Joseph (Mbosho), Comred Munuo (Kyuu), Elibariki Mbise (Rundugai), Nassor Mushi (Wari Sinde), Erasto Mushi (Kyeeri), Iddy Mtambo (Chemka), Seth Munisi (Uraa), Issa Kisanga (Kware) na Paradiso Munisi (Uswaa).

Wengine ni  Emanuel Mbowe (Nshara), Simbo Mbasha (Mungushi), Bethuel Swai (Isawerwa), Godfrey Kivuyo (Jiweni), Joel Kalungwana (Nerere), Emanuel Laizer (Mlima Shabaha), Michael Kiwelu (Kambi ya Raha), Godfrey Maimu (Umoja), Witness Mwanga (Sonu).

Akizungumza na MCL Digital leo mkurugenzi wa halmshauri ya Hai, Yohana Sintoe amethibitisha kupokea barua za kujiuzulu za wenyeviti hao.

Amesema kulikuwa na wenyeviti 19 lakini mchana ameongezeka mmoja na kufikia 20. Hata hivyo mwenyekiti huyo wa  20 jina lake halijapatikana.

"Wameeleza kujiuzulu kwa ridhaa yao kutokana na kuunga mkono Serikali," amesema Sintoe

Mkuu wa wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya amesema anawapongeza viongozi hao kwa kutumia haki yao kidemokrasia na kujiuzulu.

Sabaya amesema kwa sasa hakuna Mtanzania ambaye haoni kazi nzuri za Rais John Magufuli hivyo viongozi hao kujiuzulu wameonesha heshima kwa Rais.

"Niwapongeza kwa heshima waliyoonyesha bila kushinikizwa na mtu yoyote na mimi nawaunga mkono," amesema.