CRDB yatoa Sh150 milioni kufanikisha mkutano wa ALAT

Muktasari:

Benki ya CRDB imetoa Sh150 millioni kwa Jumuiya ya Serikali za Tawala za Mitaa na Tawala za Mikoa (ALAT) kugharamia mkutano mkuu unaotarajiwa kufanyika jijini Mwanza Julai 22, 2019.

Mwanza. Benki ya CRDB imetoa Sh150 millioni kwa Jumuiya ya Serikali za Tawala za Mitaa na Tawala za Mikoa (ALAT) kugharamia mkutano mkuu unaotarajiwa kufanyika jijini Mwanza Julai 22, 2019.

Akikabidhi hundi ya fedha hizo katika hafla iliyofanyika jijini Mwanza Julai 18, 2019, Mkurugenzi wa wateja wadogo na wa kati wa CRDB, Boma Raballa amesema msaada huo unalenga kuendeleza na kuimarisha uhusiano kati ya pande hizo mbili.

“Alat inawafikia hadi wananchi wa ngazi ya chini vijijini kama ilivyo kwa CRDB ambayo ina wateja hadi ngazi hiyo; huu ndio uhusiano tulionao unaoongeza na kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi zetu mbili,” amesema Raballa

Akipokea hudni hiyo, Mwenyekiti wa Alat Taifa, Gulamhafeez Mukadam ameishukuru benki hiyo akisema msaada huo umekuja muda mwafaka na kusema fedha hizo zitasadia kufanikisha mkutano huo muhimu unahusisha Wakurugenzi watendaji, Mameya na wenyeviti wa halmashauri, madiwani, na wakuu wa mikoa yote nchini.

Mjumbe wa kamati tendaji ya Alat, Zaynabu Vulu ambaye pia ni mbunge wa viti maalum mkoa wa Pwani ameziomba mashirika, makampuni na taasisi zingine za fedha kuiga mfano wa CRDB wa kusaidia shughuli zinazogusa maisha ya wananchi hadi ngazi za chini.