Alichosema mtoto wa dereva wa RC kabla ya kufariki

Muktasari:

Muda mfupi kabla ya kifo cha Kasobi Shida (26) aliyefariki usiku wa kuamkia juzi Jumatatu Agosti 5, 2019  katika hospitali ya Mkoa wa Mara alitaka baba yake asishtakiwe kwa kosa lolote badala yake yeye ndiye achukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria na taratibu.

Musoma. Muda mfupi kabla ya kifo cha Kasobi Shida (26) aliyefariki usiku wa kuamkia juzi Jumatatu Agosti 5, 2019  katika hospitali ya Mkoa wa Mara alitaka baba yake asishtakiwe kwa kosa lolote badala yake yeye ndiye achukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria na taratibu.

Kasobi, mtoto wa Shida Masaba (55) ambaye ni dereva wa mkuu wa mkoa wa Mara alipata ajali Agosti 4, wakati akiendesha gari linalotumiwa na baba yake kumuendesha mkuu huyo wa mkoa.

Akizungumza na Mwananchi jana katika hospitali hiyo mmoja wa maderava wenzake na baba wa marehemu ambaye hakutaka kutajwa jina, alisema kuwa alifika hospitalini hapo juzi kumjulia hali dereva mwenzie (Masaba) pamoja na kijana wake kufuatia ajali hiyo.

Dereva huyo alisema pamoja na maumivu aliyokuwa nayo kijana huyo akiongea kwa taabu alisema baba yake hastahili kuadhibiwa kwavile hakujua kama angechukua gari na kuliendesha.

Alisema baada ya kumsalimia kijana huyo alianza kulalamika huku akiulizia hali ya baba yake na kuonyesha kujutia kitendo hicho huku akiomba kuwa baba yake akipona asichukuliwe hatua kwa vile kosa alilifanya yeye.