Magufuli abadili ‘gia angani’ mkutano wa madini

Muktasari:

 

  • Rais wa Tanzania, John Magufuli leo ni mgeni rasmi katika mkutano wa sekta ya madini unaofanyika jijini Dar es Salaam ambapo ameutumia mkutano huo kuwataka wadau wa sekta hiyo kueleza changamoto mbalimbali zinazowakabili

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amebadilisha mfumo wa ratiba katika mkutano wa madini, ambapo badala ya mawaziri kuwahutubia wadau kwenye mkutano huo, amewataka wadau kutoa changamoto wanazokutana nazo ili waweze kupata suluhisho la matatizo yao.

Lengo la kufanya hivyo ni kutaka kujua kwa nini Tanzania haifaidiki kwa kuuza madini na haimo katika Benki ya Dunia (WB) kwa kuongoza katika kuuza madini hata katika nchi za Afrika Mashariki.

Mkutano huo unafanyika katika ukumbi wa kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam unashirikisha wachimbaji, wafanyabiashara na wadau wa sekta ya madini nchini.

“Tunataka tujue kwa nini madini yanatoroshwa na wanaosindikiza ni askari, tume ya madini inafanya nini katika kuhakikisha biashara hii inafanya vizuri, kwa nini Tanzanite pamoja na kujenga ukuta bado inatoroshwa, kwa nini hatuna maeneo ya soko ya madini,” amesema Rais Magufuli

“Tunataka leo tujue tunakosea wapi na kama ni mapepo wachungaji wako hapa, hivyo ni lazima makatibu wakuu, watendaji na mawaziri watueleze kwa nini,” ameongeza.

Amesema kwa maoni yake ameona hayo ndiyo ya kujadiliwa na kuangalia nani anayeanza badala ya viongozi kuwaeleza yao bila kujua changamoto za kweli.

“Ili tutoke kwenye dimbwi hili la sekta kuchangia asilimia nne tufike huko kwenye asilimia 10 mnayoitaka basi tuonyeshe uzalendo wa kweli katika sekta hii,” amesema Rais Magufuli.