Rihanna anatamani kuzaa kuliko kitu kingine maishani

Nyota wa muziki nchini Marekani Rihanna (Riri), amesema kuwa anatamani kuzaa kuliko kitu kingine kwenye maisha yake.

Riri ameyasema hayo alipokuwa akihojiwa na Sarah Paulson kwa ajili ya makala ya jarida la Interview na kudai kuwa akijipanga atatimiza ndoto yake hiyo.

Katika mahojiano hayo Riri alisema kuwa uhusiano wake na bilionea Hassan Jameel umebadili maisha yake ya kawaida, kazi zake za muziki, biashara na kujipa muda mwingi wa kupumzika.

“Anayejua ni Mungu pekee na akipenda tutafanya hivyo, ”alijibu Rihanna alipoulizwa kama watafunga ndoa na Jameel, ambaye yupo naye kwenye uhusiano kwa miaka miwili sasa.

Alisema kwa mara ya kwanza akiwa kwenye uhusiano amebaini anapaswa kuwa na muda wake binafsi, kwa sababu afya ya akili inalihitaji hilo.

“Kama hauna furaha, huwezi kuwa na furaha hata ukifanya kitu unachokipenda. Ninataka kufanya kazi kama starehe, sitaki kufanya kazi adhabu, ”alisema.

Alisema kuna vitu amevifanya vimekuwa rahisi, anaamua kwenda kazini au kupata kinywaji.

Alifafanua anajipa mapumziko ya siku mbili au tatu kwa ajili ya mambo binafsi na wameanzisha kitu kipya kwenye uhusiano wao kinaitwa kwa kifupi ‘P’ kikimaanisha “personal days”.