Rais Putin asogeza mbele kura mabadiliko ya Katiba

Muktasari:

Awali kura hiyo ya mabadiliko ya Katiba ilipangwa kufanyika Aprili 22, ambako pamoja na mambo mengine inamuwezesha Rais Vladmir Putin kugombea tena nafasi hiyo kwa muhula mwengine.

Moscow, Urusi. Rais wa Urusi, Vladmir Putin ameahirisha kura ya maoni ya mabadiliko ya Katiba yenye lengo la kuongeza madaraka kwa kipindi kingine.

Katika hotuba yake kwa njia ya televisheni Putin alisema amehairisha kura hiyo kutokana na athari za virusi vya corona.

Hata hivyo, kiongozi huyo ambaye yuko madarakani kwa zaidi ya miongo miwili sasa hakuweka wazi ni lini hasa kura hiyo itafanyika.

Mabadiliko hayo ya Katiba pamoja na mambo mengine yanaondoa marufuku ya kikatiba dhidi ya Rais huyo kugombea tena mwaka 2024 na sasa ataruhusiwa kugombea tena kwa vipindi viwili.

Awali mabadiliko hayo yaliyopitishwa na Bunge la juu na Mahakama ya kikatiba nchi Urusi yalipangwa kuidhinishwa kwa kupigiwa kura Aprili 22.

Lakini jana Rais Putin alisema kuwa suala la kipaumbele kwa taifa sasa ni afya, uhai na usalama wa watu.