Bendi tisa za muziki wa dansi kutumbuiza Dar

Muktasari:

Kuelekea maadhimisho ya kumbukizi ya kifo cha baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, bendi tisa zitatumbuiza kutoa burudani itakayoambatana na utoaji ujumbe kuhusu thamani ya amani, umoja na upendo iliyorithishwa na waasisi wa Taifa.

 


Dar es Salaam. Bendi tisa za muziki wa dansi nchini Tanzania zitatoa burudani katika Tamasha la Mwalimu 2019, katika viwanja vya Mwembe Yanga, Temeke jijini Dar es Salaam.

Tamasha hilo litafanyika  Septemba 12, 2019 ikiwa ni maadhimisho  ya miaka 20 tangu kifo cha Rais wa kwanza Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere. Mwalimu Nyerere alifariki Oktoba 14 mwaka 1999 jijini London nchini Uingereza  alikokuwa amekwenda kwa matibabu.

Hayo yamesemwa  leo Jumatano Septemba 4, 2019 na  Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi, Simon Mwakifwamba ambapo amesema tamasha hilo kabla ya maadhimisho rasmi ya kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere yatakayofanyika kitaifa Mkoani Lindi Oktoba 14, 2019.

Mwakifwamba amezitaja bendi hizo kuwa ni African Stars 'Twanga Pepeta' TOT, Sikinde, Msondo, Malaika Bendi, Mambo Live, Vijana Jazz, Ivory Band na Double M Sound.

Amesema  wameamua kutumia sanaa kuwakumbusha vijana thamani ya amani, umoja na upendo uliorithiwa  kutoka kwa mashujaa na waasisi wa Taifa.

Amefafanua mbali na muziki wa bendi kutakuwepo pia na burudani za vichekesho  kutoka kwa wachekeshaji mahiri zaidi ya 10 akiwemo Oscer Nyerere, Babu Ayubu, Mlugaluga na  Max the great.