Hizi zinaweza kuwa sababu za Harmonize kutaka kujitoa Wasafi

Muktasari:

Inawezekana Harmonize anataka kuondoka katika kundi la Wasafi kwa sababu nyingine  lakini kuweza kufanya mambo mbalimbali ambayo msanii hupaswa kuwa nayo huenda ikawa sababu kubwa ya kutamani kufanya muziki nje ya kundi hilo


Dar es Salaam. Kitendo cha msanii Harmonize kuandika barua kutaka kujitoa katika kundi la Wasafi kinaashiria kuwa amedhamiria kupambana mwenyewe.

Huo ndio ukweli kwa  kuwa meneja wa kundi hilo, Sallam ameeleza kuwa msanii huyo ameandika barua ya kuomba kuvunja mkataba na kundi hilo.

Lakini kabla ya Sallam kubainisha jambo hilo jana Jumatano Agosti 21, 2019 katika mahojiano na televisheni ya Wasafi, Harmonize alikuwa ameanza kuonyesha dalili za kujiondoa katika kundi hilo.

Kwa sasa Harmonize anamiliki studio kubwa ya muziki iliyopo Sinza jijini Dar es Salaam.

Harmonize pia alijipanga kwa kuwa na lebo ya muziki  ya Konde Gang ambayo inafanya kazi zake kama ilivyo Wasafi, si rahisi kuendelea kufanya kazi kwenye lebo nyingine ilihali anayo ya kwake.

Pia amekuwa akipata mialiko ya kazi zake binafsi badala ya kupitia lebo ya Wasafi.

Hivi karibuni alibadili maelezo katika ukurasa wake wa Instagram na kuondoa maneno yaliyoashiria anafanya kazi chini ya Wasafi na kuweka namba kwa ajili ya miadi ya shoo tofauti ambazo awali zilikuwa zitapitia Wasafi.