Makundi ya wasanii Tanzania yaikataa Cosota

Muktasari:

Makundi ya wasanii yaliyokutana kwa ajili ya kujadili maelekezo ya Waziri wa Habari Dk Harison Mwakyembe aliyewapa siku 14 kujadili lengo la kuunganisha Cosota, Basata na Bodi ya Filamu. Hata hivyo, alikataa Cosota kuunganishwa na taasisi hizo mbili.


Dar es Salaam. Majadiliano ya takribani saa sita kutafuta mwarobaini wa kufuta machozi ya wasanii nchini Tanzania yaliyodumu miongo kadhaa jana Jumatano Agosti 28,2019 ulipitiwa na ‘bundi’ baada ya wasanii hao kupinga vikali hoja ya kuunganisha Chama Hakimiliki Tanzania (Cosota), Bodi ya Filamu na Baraza la Sanaa la  Taifa  (Basata).

Hata hivyo, wasanii hao wakiwamo wa filamu na muziki wamesema huenda pendekezo hilo la Serikali ya Tanzania likaota ‘mbawa’ baada ya kutaka Basata na Bodi ya filamu na kuikataa Cosota.

Mara baada ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe ambaye aliongozana na Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa kuzungumza aliwapa wasanii hao siku 14 kuwasilisha mapendekezo yao.

Aliwataka wasanii hao wajadiliane kisha kuwasilisha mapendekezo ya mjadala huo kwa ajili ya kuyafanyia kazi. 

Katibu Mkuu wa Chama cha Muziki wa Dansi Tanzania (Chamudata) Hassani Msumari alisema “Wizara na wataalamu kwa vilio vyetu vingi huko nyuma tulikuwa tukiomba viunganishwe kuondoa ukiritimba, sasa hili la filamu na Basata halina hoja.”

“Ila Cosota wengi hata mimi kuunganisha hatutaki hata sheria za dunia za haki miliki hazitaki,” alisema.

Alisema haafiki kwa kuwa makusanyo ya mirabaha ni fedha zinazotakiwa moja kwa moja ziwafikie wadau wanachama, lakini hawaelewi namna Cosota inavyolifanyia kazi suala hilo.

Hoja nyingine ya Msumari ni kwamba Sheria za haki Miliki/Shiriki duniani zinaitaka mifuko au asasi (cosota  kujitegemea kama ilivyo FIFA. “Tambua haki miliki ni sheria za dunia (w.i.p.o)would intellectual propert organization”

“Tutakuwa wa ajabu tukiichanganya Cosota na Serikali, ambayo imeonyesha nia ya kuondolea udhalimu wa muda mrefu, “amesema Francis Kaswahili, mwanzilishi wa hakimiliki Tanzania.”

 

“Tukio hilo halitawezeka kuwepo kwenye Serikali ila haya mambo mawili Basata na Bodi ya filamu ndio watengenezewe muundo wa pamoja” amesema Ras Innocent Nganyagwa

 “Cosota haiwezi kuchanganywa na huo utatu, bora tubakie na bodi ya filamu na Basata,” alisema Ado Novemba rais wa Shirikisho la Muziki wa Injili (TAF)

Naye rais wa Shirikisho la Filamu nchini, Simon Mwakifamba alisema kuwa haoni haja ya kuunganishwa Cosota na hizo taasisi nyingine kwa sababu wao ndiyo wanapaswa kusimamia maslahi ya wasanii, japokuwa hakuna kilichofanyika hadi sasa.