Marekani yatangaza ushuru bidhaa za Brazil, Argentina

Muktasari:

Rais huyo wa Marekani alizituhumu nchi hizo kuongoza katika kushusha thamani ya sarafu zao hatua ambayo inawaumiza wakulima wa Marekani.


Washington, Marekani. Rais wa Marekani, Donald Trump ametangaza nchi yake kutoza ushuru kwa bidhaa za chuma na alumini zinazoagizwa kutoka Brazil na Argentina.

Rais Trump alisema hayo kupitia ukurasa wake wa Twitter jana Jumatatu Desemba 2.

Trump alisema Brazil na Argentina zimekuwa zikiongoza katika kushusha thamani ya sarafu zao hatua ambayo inawaumiza wakulima wa Marekani.

Kiongozi huyo alienda mbali zaidi na kuitaka Benki ya Dunia (WB) kuchukua hatua kali ili mataifa mengine yasitumie vibaya uimara wa dola ya Marekani katika kuzishusha thamani sarafu za nchi zao.

Mwaka jana Rais Trump alitangaza nyongeza ya ushuru wa asilimia 25 katika bidhaa za chuma na 10 katika alumini.

Hata hivyo, Machi mwaka huu Rais huyo machachari alitangaza tena kuondoa ushuru huo kwa nchi za Argentina na Brazil pamoja na nchi nyingine ambazo awali zilikuwa zimejumuishwa.

Akizungumzia hatua hiyo ya Trump, Rais wa Brazil, Jair Bolsonaro alisema amepanga kukutana na kiongozi ili kujadili suala hilo.