Mwanafunzi ajiua kwa kujipiga risasi

Muktasari:

Mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Arusha Meru, Faisal Salimu (19) amejiua kwa kujipiga risasi jana Jumapili Agosti 18.


Arusha. Mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Arusha Meru, Faisal Salimu (19) amejiua kwa kujipiga risasi jana Jumapili Agosti 18.

Mwanafunzi huyo amejipiga risasi kwa kutumia bunduki ya baba yake Salimu Ibrahim (59) aina ya Rifle Winchester akiwa amejifungia chumbani kwake katika nyumba ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) eneo la Soko Kuu jijini Arusha nchini Tanzania.

Kamanda wa polisi mkoa wa Arusha, Jonathan Shani amesema katika tukio hilo lilitokea Jumapili saa 11 alfajiri, mwanafunzi huyo alijipiga risasi katika paji la uso.

Uchunguzi wa awali umebaini mwanafunzi huyo alikuwa anasumbuliwa na msongo wa mawazo kutokana na kushutumiwa kuwa anatumia dawa za kulevya.

"Tumeanza uchunguzi wa tukio hili na silaha hii kama ilikuwa inamilikiwa kihalali. Hatua za kisheria zitachukuliwa ikibainika kama silaha haikuhifadhiwa vizuri," amesema Shana.

Jirani wa nyumba huyo, Ahmed Issa amesema mwanafunzi huyo alifariki akiwa njiani wakati anapelekwa katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mountmeru.

"Tukio hili lilifanywa siri sana, hata sisi majirani tumepata taarifa usiku huu," amesma jirani huyo.