Ndugai: Orodha shughuli za Bunge kutolewa kwa njia ya kimtandao kumeokoa Sh63 milioni
Muktasari:
Spika Job Ndugai amesema uamuzi wa Bunge la Tanzania kuachana na utaratibu wa kutoa orodha ya shughuli zake za siku katika makaratasi, na kuhamia katika njia ya mtandao wa WhatsApp na email utaokoa Sh63 milioni kwa mwaka.
Dodoma. Spika Job Ndugai amesema uamuzi wa Bunge la Tanzania kuachana na utaratibu wa kutoa orodha ya shughuli zake za siku katika makaratasi, na kuhamia katika njia ya mtandao wa WhatsApp na email utaokoa Sh63 milioni kwa mwaka.
Ndugai ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Septemba 12, 2019 katika uzinduzi wa teknolojia ya kidijitali itakayotumika katika shughuli za Bunge.
Amesema matumizi ya karatasi yanasababisha gharama kuwa kubwa, akitolea mfano mikutano minne ya Bunge yenye vikao 88.
Amesema orodha ya shughuli za Bunge kwa siku zinatumika karatasi 12 kwa mtu mmoja, hutolewa orodha 600 kwa ajili ya wabunge, watumishi na wadau wengine.
Amesema kwa mwaka wamekuwa wakitumia karatasi 633,600 ambazo pamoja na mambo mengine hugharimu Sh63 milioni.