Polisi yawakamata raia wanne wa kigeni

Kamand wa polisi mkoabwa Dodoma Gilles Muroto akionyesha pikipiki zilizokuwa zikiwasafirisha wahamiaji kutoka nchini Ethiopia na Somalia... Kulia ni madereva was pikipiki hizo ambao ni raia wa Tanzania

Muktasari:

Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma linawashilia raia wanne wa Ethiopia na Somalia kwa madai ya kuingia nchini Tanzania kinyume na sheria.

Dodoma. Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma linawashilia raia wanne wa Ethiopia na Somalia kwa madai ya kuingia nchini Tanzania kinyume na sheria.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Oktoba 24, 2019 kamanda wa polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amesema wahamiaji hao walikamatwa wilayani Mpwapwa wakitoka Arusha kuelekea Iringa wakiwa katika pikipiki.

Amesema polisi pia wanawashikilia Watanzania wawili waliokuwa wakiwasafirisha raia hao wa kigeni kutoka Arusha kwenda Iringa.

Amewataja watu hao kuwa ni Sellamu Yohanes na Ashetu Tefaye (Waethiopia), Mahamoudu Mapaa na Cuse Ciise (Wasomali). Amesema Watanzania waliokamatwa ni Jamali Martin na Wiston Makia.

“Pia watuhumiwa walikuwa na Sh1 milioni walizokuwa wamepanga kuwahonga askari wetu ili wasiwakamate lakini walikataa rushwa hiyo,” amesema Muroto.