Profesa Ndalichako atoa angalizo matumizi ya teknolojia kwa watoto

Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akifungua kongamano la saba la tafiti linalolenga kuangalia elimu ya awali, makuzi na maendeleo ya mtoto lililofanyika jijini Dar es Salam jana lililoandaliwa na Chuo Kukuu cha Aga Khan (AKU). Picha na Salim Shao

Muktasari:

Waziri wa Elimu nchini Tanzania amewataka wazazi kuwa makini na watoto wao katika matumizi ya teknolojia ili kuwaepusha na mambo yasiyo muhimu kwao.

Dar es Salaam. Waziri wa Elimu nchini Tanzania amewataka wazazi kuwa makini na watoto wao katika matumizi ya teknolojia ili kuwaepusha na mambo yasiyo muhimu kwao.

Amesema teknolojia inaweza kutumika kwa ajili ya kuwafundisha watoto, kutaka iwe sahihi kwa umri wao.

Ametoa kauli hiyo leo Jumatano Desemba 4, 2019 katika ufunguzi wa kongamano la saba la tafiti linalolenga kuangalia elimu ya awali, makuzi na maendeleo ya mtoto.

“Dunia ya sasa ni ya sayansi na teknolojia, wakati mwingine tunapata  changamoto ya teknolojia kufundisha watoto, zipo teknolojia tunatakiwa kuwa nazo makini kwa watoto wetu, zitengenezwe ambazo ni sahihi na kuwajenga,” amesema Profesa Ndalichako.

Kongamano hilo lililoandaliwa na Chuo Kukuu cha Aga Khan (AKU) limeshirikisha watafiti kutoka mataifa mbalimbali ikiwemo nchi za Afrika Mashariki litakuja  na pendekezo la pamoja ya kuangalia namna ya kuboresha elimu ya awali.

Amesema  elimu ya awali ni muhimu kwa maendeleo ya watoto kwa sababu inamsaidia kukuza akili yake

“Nimefurahi kuona AKU mmeweka umuhimu kuzungumzia elimu ya awali ambayo ni msingi mzuri kwa mtoto.”

“Serikali ipo tayari kupokea mapendekezo yatakayotolewa na wadau na kuyafanyia kazi kukuza elimu ya awali kwa sababu lengo la kuimarisha elimu hii ni kupata watoto wenye uelewa, nidhamu kwa sababu tunataka Taifa imara,” amesema Ndalichako.

Mtaalamu wa elimu ya awali wa AKU,  Dk Shelina Walli amesema jamii haiipi kipaumbele elimu ya awali, kwamba mkutano huo utakuja na mapendekezo kuhusu elimu hiyo.