Sababu kampeni wanawake kumiliki ardhi yatajwa

Muktasari:

Kampeni ya kupigania haki ya mwanamke kumiliki ardhi nchini Tanzania inatarajiwa kuzinduliwa kesho na kuendelea kwa miaka 12 mfululizo.

Dar es Salaam. Kampeni ya kupigania haki ya mwanamke kumiliki ardhi nchini Tanzania inatarajiwa kuzinduliwa kesho na kuendelea kwa miaka 12 mfululizo.

Kampeni hiyo ya ‘linda ardhi ya mwanamke’ itahusisha  asasi 26 zinazojishughulisha na masuala ya ardhi. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu atakuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo.

Hayo yameelezwa leo Jumatano Novemba 20, 2019 na mwenyekiti wa kampeni hiyo, Tike Mwambipile wakati akitangaza kuanza kwa kampeni hiyo iliyojikita katika maeneo manne ikiwa ni pamoja na kuondoa mila na desturi kandamizi zinazowakwamisha wanawake kupata haki zao katika ardhi.

“Lakini pia tumelenga kuwawezesha wanawake kutumia ardhi zao kwa manufaa hasa ya kiuchumi, kuongeza ushiriki wa wanawake katika vyombo vya kutoa uamuzi  pamoja na kulinda haki za mwanamke katika ardhi hasa katika maeneo yenye uwekezaji wa ardhi.”

“Tunataka mwisho wa kampeni hii tuone matokeo chanya ikiwemo zaidi ya asilimia 60 ya wanawake kuwa na uwezo wa kudai haki zao katika ardhi na kuboresha maisha yao ya kiuchumi,” amesema.

Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari wanawake (Tamwa), Rose Reuben amesema wakati mwingine ardhi zimekuwa zikiuzwa kiholela kwa sababu wanawake ya wanawake kutohesabika katika umiliki.