VIDEO: Tanzania kuongoza ushawishi China iwekeze Sadc

Muktasari:

  • Ingawa China imetenga Dola 60 bilioni zitakazowekezwa Afrika kwa miaka mitano, nchi za Sadc zinatanua wigo kwa kuwakaribisha wafanyabiashara na wawekezaji kutoka China kuja kuwekeza zaidi Afrika ndani ya wanachama wa Sadc.

Dar es Salaam. Baada ya kumalizika kwa mkutano mkuu wa 39 wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc), ubalozi wa Tanzania umeandaa mkutano wa kuwakaribisha wawekezaji kuchangamkia fursa zilizopo.

Mkakati huo wa kukaribisha wawekezaji unafanywa na mabalozi wote kutoka nchi 16 za Sadc waliopo China ambao kwa pamoja, watakutana na wafanyabiashara wakubwa pamoja na wawakilishi wa Serikali.

Balozi wa Tanzania nchini China, Mbelwa Kairuki anasema baada ya kutoka kwenye mkutano wa Sadc uliofanyika Agosti 2019 jijini Dar es Salaam nchini Tanzania kisha kurudi kwenye kituo chao cha kazi, mabalozi hao waliweka mkakati wa pamoja.

"Huu ni mkakati wetu mabalozi wa Sadc tuliopo China chini ya uenyekiti wa Tanzania. Oktoba 28, 2019 tutakuwa na mkutano mkubwa kuwaonyesha wafanyabiashara fursa tulizonazo," amesema Balozi Mbelwa.

Mkutano huo, amesema utafanyika katika Jiji la Nanjing ambalo ni la pili kwa uchumi mkubwa nchini humo likiwa na pato (GDP) la Dola 1.4 trilioni likiwa nyuma ya Jiji la Guandong.