Waziri Mkuu akoleza uchaguzi serikali za mitaa

Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa

Muktasari:

Serikali imetangaza kuwa uchaguzi wa serikali za mitaa uko palepale licha ya malalamiko mengi kutaka usifanyike.

Dodoma. Hakuna kulala uchaguzi wa serikali za mitaa uko palepape.

Ndivyo unavyoweza kusema baada ya kauli ya Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa kuliambia Bunge leo Ijumaa Novemba 15, 2019 kuwa Watanzania wajitokeze kwa wingi katika uchaguzi huo utakaofanyika Novemba 24, 2019.

Akitoa hotuba ya kuahirisha mkutano wa 17 wa Bunge, Majaliwa amesisitiza Watanzania kujitokeza na kuwachagua viongozi wanaowapenda kwa ajili ua kuwatumikia.

Baadhi ya vyama vya siasa na wanaharakati wamekuwa wakilalamikia dosari kadhaa katika uchaguzi wakiomba usitishwe ili vyama vijadiliane.

Vyama vingine vimetangaza kujitoa katika uchaguzi huo na kuomba majina na nembo za wagombea wao visitumike kwenye uchaguzi huo.

Katika maeneo mengi, chama tawala cha CCM kimepita bila kupigwa katika vitongoji, mitaa na vijiji kutokana na sababu mbalimbali.

Vyama vilivyokwisha kutangaza kususia uchaguzi huo ni; Chadema, CUF, ACT- Wazalendo, NCCR-Mageuzi, NLD, UPDP na Chaumma.