Zuchu atua mikononi mwa Joeboy wa Nigeria

Muktasari:

Zuchu anakuwa msanii wa kwanza Tanzania kuachia ngoma kumshirikisha Joeboy ambaye hivi karibuni alikuja nchini kwa ajili ya shughuli za muziki.

Dar es Salaam. Msanii anayekuja kwa kasi kutoka lebo ya muziki ya Wasafi,  Zuchu ameachia wimbo mpya leo ikiwa ni kwa mara ya kwanza amemshirikisha msanii kutoka nje ya nchi.

Wimbo huo ulioachiwa leo Oktoba 16 umepewa jina la ‘Nobody’, na umeimbwa na Zuchu ambaye jina lake halisi ni  Zuhura Othman, akimshirikisha Joeboy, msanii kutoka Nigeria ambaye ametamba na ngoma kali kama vile Beginning na Baby.

Mashairi katika wimbo huo yanahusu wapenzi wawili, mwanamke na mwanaume wakielezeana jinsi kila mmoja anavyompa raha mwenzake kwenye penzi lao, kiasi kwamba hata wakijaribu kilinganisha, hakuna mtu aliyewahi kuwafanyia kwa namna hiyo na wala hatotokea.

Wimbo umetengenzwa na prodyuza Tony na Laizer wa Wasafi huku video ikiongozwa na director Kenny wa Zoom Extra inayomilikiwa na Diamond Platnumz.

Mfahamu Joeboy

Joeboy ni msanii wa Nigeria ambaye amevuma kwa ngoma maarufu za Baby na Beginning. Mbali na kuimba, kingine kilichompa umaarufu Joeboy ni staili ya utengenezaji wa video za nyimbo zake kwa mtindo wa vikatuni.