Serikali yakumbusha usimamizi wa miradi ya maendeleo
Muktasari:
- Serikali imesema itawachukulia hatua viongozi watakaohujumu na kukwamisha usimamizi wa miradi ya maendeleo katika halmashauri zote nchini.
Hai. Serikali imesema itawachukulia hatua viongozi watakaohujumu na kukwamisha usimamizi wa miradi ya maendeleo katika halmashauri zote nchini.
Hayo yamesemwa leo Alhamisi Februari 11, 2021 na Naibu Waziri wa Tamisemi, David Silinde wakati akizindua jengo la afya ya kinywa na meno hospitali ya Wilaya ya Hai lililogharimu zaidi ya Sh82 milioni.
Silinde amesema Halmashauri nyingi nchini zinashindwa kusimamia vyema miradi ya maendeleo badala yake zinatumia fedha za miradi kwa manufaa yao na kukwamisha azma ya serikali.
"Halmashauri nyingi nchini kwenye mpango wa usimamizi wa miradi wamekuwa wakifeli ndio maana baada ya Rais Magufuli (John) kuingia madarakani akatutoa kwenye mfumo wa awali wa wazabuni akatupeleka kwenye akaunti ambapo watu walipata nafasi ya kutandika fedha kwelikweli.”
"Usimamizi wa fedha ndio wajibu wetu namba moja ,tukileta fedha isimamieni ifanye kazi yake iliyokusudiwa na iishe na isipokamilika ipasavyo tutamchukulia msimamizi hatua kali za kinidhamu kwa kushindwa kutekeleza wajibu wako wa kuhakikisha unasimamia vyema miradi ya Serikali," amesema Silinde
Amesema, “safari hii fanyeni kazi kadri inavyowezekana maana mimi kukusimamisha kazi siogopi wala sijali, tufanya kazi bila kumwonea mtu na tutatenda haki, atakayefanya vizuri tutampongeza na atakayefanya vibaya tutamchukulia hatua.”