1,000 wajitosa kuwania nafasi 10 za ajira

1,000 wajitosa kuwania nafasi 10 za ajira

Muktasari:

  • Kampuni ya PanAfrican Energy Tanzania (PAET) imesema, imekuwa ikipokea maombi 1,000 kila mwaka kwa ajili ya mchujo wa nafasi kumi kupitia programu ya ajira kwa vitendo.

Dar es Salaam. Tatizo la ajira nchini limeendelea kuonekana kwa watalaamu wanaozalishwa sekta ya gesi, baada ya Kampuni ya PanAfrican Energy Tanzania (PAET) kupokea maombi ya wahitimu 1,000 kwa ajili ya mchujo wa nafasi kumi zinazohitajika kila mwaka kupitia programu ya ajira kwa vitendo.

 Kauli hiyo imetolewa leo Agosti 4, 2022 Jijini Dar es Salaam wakati wa Kongamano la Kimataifa la Nishati 2022, linalofanyika kwa awamu ya nne likiwa na kampuni 100 za kimataifa na wageni kutoka mataifa 25.

Katika tukio hilo, Meneja Rasilimali Watu wa Kampuni hiyo, Gasper Mkomba amesema asilimia 40 ya waombaji hukosa sifa hatua inayowalazimu kujikita katika asilimia 60 ya waombaji.

“Waombaji ni wengi sana kwa kweli, lakini proramu inahitaji kumi tu,  tumeanza mwaka huu na tutaifanya hadi mwaka 2025, tutakuwa tunachukua watalaamu kumi kila mwaka wa kozi za uhandisi wa Petroli, uhasibu, utawala, uhandisi wa kimazingira, Lojistiki, “amesema Mkomba.

“Katika asilimia 60 ndio wanakuwa angalau wamezigatia vigezo, lakini tunachukua 70 tu kati yao ambao tunawachuja hadi 40 katika usaili wa kwanza. Usajili wa pili tunapata 20 na usaili wa tanapata hao 10. Wakiajiriwa wananufaika na ujuzi, mishahara na vyeti vya kutambuliwa baada ya kumaliza mwaka.”

Katika ufafanuzi wake, Mkomba amesema kampuni hiyo inaamini hatua hiyo itawajengea uwezo na uzoefu wa kuajirika kwa urahisi katika fursa mbalimbali za sekta hiyo kwa miaka ijayo.