Afungwa maisha gerezani kwa kumbaka mtoto wa miaka sita

Songwe. Mkazi wa Ilembo, Kata ya Vwawa wilayani Mbozi Mkoa wa Songwe, Betwel Anyalwisye (51), amehukumiwa kifungo cha maisha gerezani baada ya kukutwa na hatia ya kumbaka mtoto mwenye umri wa miaka sita.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu wa mahakama ya wilaya ya Mbozi, Names Chami amesema Mahakama imemtia hatiani mshitakiwa baada ya kujiridhisha na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka pasipo kuacha shaka yoyote.

Chami amesema mtuhumiwa alitenda kosa hilo Agost 6, 2022 katika maeneo ya Ilembo kata ya Vwawa kwa kumbaka mtoto wa miaka sita huku akijua kufanya hivyo ni kosa na ni  kinyume na kifungu cha sheria cha 130(1)na (2)e na kifungu cha 131 (3) sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16.

Amesema mahakama baada ya kujiridhisha na ushahidi inamhukumu Betwel Anyalwisye kutumikia kifungo cha maisha gerezani ili liwe fundisho kwa watu wanaofanya vitendo hivyo kwa wilaya ya Mbozi na Taifa kwa ujumla.

“Mtuhumiwa alikuwa akifanya tendo hilo mara kadhaa lakini Agost 6, 2022 alikamatwa katika kitongoji cha Ilembo ilipo nyumba yake baada ya kumdanganyishia kwa kumpa zawadi ya pipi mtoto mdogo mwenye miaka sita na kufanya uovu huo wa kikatili kwa mtoto,’’ amesema Chami.

Awali, imedaiwa mahakamani hapo na mwendesha mishitaka wa Polisi, Ally Kambona mtuhumiwa alikuwa akimfanyia ukatili huo mtoto huyo mara kwa mara huku akimdanganyishia zawadi mbalimbali hasa pipi na biskuti.

Amesema mtuhumiwa alikamatwa Agost 6, 2022, baada ya ushirikiano walioutoa majirani waliobaini vitendo vya mtuhumiwa huyo, ambapo siku hiyo alimrubuni mtoto huyo na kwenda kulala naye nyumbani kwake.

“Siku ya tukio mtoto huyo hakurudi nyumbani, wakiwa katika harakati za kumtafuta mtoto huyo aliyetoweka muda wa jioni, asubuhi walimuona akitoka nyumbani kwa mtuhumiwa ambapo baada ya majirani na wazazi kumhoji mtoto huyo alisema amekuwa akienda mara kwa mara kwa mtuhumiwa huku akizawadiwa zawadi mbalimbali hasa pipi,” amesema Kambona.

Kambona ameiomba Mahakama kutoa adhabu kali ambayo itakuwa fundisho kwa wale wote wenye tabia za kuwafanyia ukatili watoto wadogo  kwa kuwarubuni watoto wadogo na kulala nyumbani kwake mpaka asubuhi.

Akizungumza nje ya Mahakama, afisa ustawi wa jamii wilaya ya Mbozi, Daudi Mdaki amesema walipo pata taarifa za tukio hilo la kikatiri kwa wasamalia wema walifuatilia wakishirikiana na jeshi la polisi na kufanikiwa kumfikisha mtuhumiwa mahakamani.

Amesema ndugu na majirani walitoa ushirikiano mzuri ambao umesababisha kufanikiwa kwa kesi hiyo tofauti na matukio mengine ambayo ndugu na majirani huficha na kufanya makubaliano pindi unapotokea ukatili kwa watoto.