Askari adaiwa kuua mhudumu wa baa kisa bili
Muktasari:
- Konstebo wa Polisi adaiwa kumfyatulia risasi mhudumu wa baa, ni baada ya kupewa bili ya Sh261,107
Kenya. Konstebo wa Polisi, Nicholas Masau anashikiliwa na jeshi hilo akituhumiwa kumuua mhudumu wa baa na kujeruhi wengine wanne.
Tukio hilo limetoka Desemba 13, 2023 Nakuru Kenya.
Askari huyo alizua kizaazaa katika Baa ya Vegas alipopelekewa bili ya Ksh16,000 (Sh261,107).
Tovuti ya Tuko imesema askari huyo alikimbia baada ya kufyatua risasi na kumuua mhudumu huyo, huku watu wengine wakijeruhiwa.
“Alizua ugomvi na wahudumu wa baa kutokana na bili za vinywaji alivyokunywa. Hali ya sintofahamu ilitokea, akamfyatulia risasi mhudumu wa baa ambaye ni Ann Maina,” imeeleza ripoti.
Kamanda wa Polisi Kaunti ya Nakuru, Samuel Ndanyi, amesema Masau alikamatwa na kuzuiwa katika kituo cha polisi cha Kaptebwa. Amesema bastola yenye risasi mbili imepatikana.
Polisi wamesema katika tukio hilo majeruhi ni wanaume wawili na wanawake wawili.
Mwili wa Ann umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti, kusubiri uchunguzi.