Biden kuanza kutaja mawaziri wake Jumanne

Biden kuanza kutaja mawaziri wake Jumanne

Muktasari:

Mashirika kadhaa ya habari ya Marekani, likiwemo Bloomberg na The New York Times, yameripoti kuwa rais-mteule atamtangaza mwanadiplomasia maarufu na msaidizi wake wa muda mrefu, Antony Blinken kuwa waziri wa mambo ya nje. 

Washington, Marekani (AFP)
Rais wa Marekani, Joe Biden atatangaza wateule wake wa kwanza katika baraza la mawaziri kesho, mnadhimu wake mkuu alisema, licha ya Donald Trump kuendelea na madai yasiyo na ushahidi kuhusu udanganyifu huku hali ya upinzani ikiendelea kukua ndani ya chama chake.
Biden ameendelea na maandalizi ya kuchukua nchi ifikapo Januari 2020, bila ya kujali mpango wa Trump wa kupindua matokeo ya kura zilizopigwa mwezi huu.
"Mtaona wateule wa kwanza wa baraza la mawaziri Jumanne," mnadhimu huyo wa Biden, Ron Klain, alisema katika kipindi cha "This Week" kilichorushwa na kituo cha televisheni cha ABC jana Jumapili (Novemba 22).
Mashirika kadhaa ya habari ya Marekani, likiwemo Bloomberg na The New York Times, yameripoti kuwa rais-mteule atamtangaza mwanadiplomasia maarufu na msaidizi wake wa muda mrefu, Antony Blinken kuwa waziri wa mambo ya nje.
Biden pia alisema wiki iliyopita kuwa ameshaamua mteule wake wa nafasi muhimu ya waziri wa fedha.
Vyombo vya habari vya Marekani pia viliripoti kuwa Biden atamteua Linda Thomas-Greenfield, ambaye alikuwa msaidizi wa waziri wa mambo ya nje anayeshughulikia Afrika chini ya Rais Barack Obama, kuwa balozi wa Marekani Umoja wa Mataifa.

Wakati Trump akikataa kukubali matokeo ya uchaguzi, Biden na wasaidizi wake wa karibu wamezuiwa kuzungumzia masuala nyeti ya nchi na ya kimataifa,  hasa suala la ugonjwa wa virusi vya corona linaloiumiza nchi.