Bilioni 985 za WB kutumika mradi kuboresha elimu ya juu Tanzania

New Content Item (1)
New Content Item (1)

Muktasari:

Zaidi ya Dola milioni  425 za Marekani (zaidi ya Sh985.1 bilioni) za mkopo kutoka Benki ya Dunia (WB) zitatumika kutekeleza mradi wa kuboresha elimu ya juu kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa Tanzania.

Dar es Salaam. Zaidi ya Dola milioni  425 za Marekani (zaidi ya Sh985.1 bilioni) za mkopo kutoka Benki ya Dunia (WB) zitatumika kutekeleza mradi wa kuboresha elimu ya juu kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa Tanzania.

Mradi huo unaotarajiwa kutekelezwa katika kipindi cha miaka mitano na Serikali utaanza katikati ya mwaka 2021.

Kupitia mradi huo kutafanyika uboreshaji miundombinu ya kujifunza na kufundishia, kununua vifaa vya kisasa ikiwemo vya maabara, kuendeleza wanataaluma.

Akizungumza leo Jumatano Januari 14, 2021 katika mkutano wa wadau uliokuwa umelenga kujadili rasimu ya miongozo ya utekelezaji wa mradi huo, katibu mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk Leonard Akwilapo amesema mradi huo unakuja kujibu changamoto katika elimu ya juu nchini.

Amesema matarajio ya Serikali sasa ni vyuo vikuu kutozalisha wahitimu ambao si wataalamu wa chochote bali wawe walio na ujuzi wa kuweza kujiajiri na kuajirika

“Mitaala yote ilenge soko nyumbulifu kwa kadri ya mabadiliko ya teknolojia, mradi huu utaleta mapinduzi au mageuzi katika elimu ya juu kwa ajili ya kujenga uchumi wa kisasa,” amesema Dk Akwilapo

Amebainisha kuwa mradi huo unalenga kutambua mahitaji ya nchi na kujibu changamoto ambazo sekta elimu ya juu inakutana nazo.

“Yanatakiwa kufanyika maboresho na mageuzi makubwa katika mfumo wa utoaji wa elimu ya juu nchini ambayo yatasababisha kuwepo kwa mabadiliko chanya katika nyanja zote zinazohusiana na ukuzaji wa uchumi wa nchi,” amesema Dk Akwilapo.