Watu sita wa familia moja wauawa Kigoma
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Menrad Sindano akizungumzia mauaji ya watu sita wa familia moja waliouawa usiku wa kuamkia leo Jumapili Julai 3, 2022 katika Kijiji cha Kiganza wilayani Kigoma.
Muktasari:
- Watu sita wa familia moja wameua kwa kukatwa na kitu chenye ncha kati sehemu mbalimbali za miili yao katika kijiji cha Kiganza wilayani Kigoma, mkoani Kigoma usiku wa kuamkia leo Jumapili Julai 3, 2022
Kigoma. Watu sita wa familia moja wameuawa kwa kukatwa sehemu mbalimbali za miili yao kwa kitu chenye ncha kali na watu wasiojulikana katika Kijiji cha Kiganza wilayani Kigoma mkoani Kigoma.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Menrad Sindano amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo Jumapili Julai 3, 2022.
Sindano amesema katika mauaji hayo watoto wawili wamejeruhiwa, mmoja mwenye miezi mitatu na mwingine mwenye umri wa miaka minne, ambao kwa sasa wanapatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Maweni.
Amesema Jeshi la Polisi linaendelea na msako mkali kuweza kuwabaini watu waliofanya mauaji hayo na kwamba hatua kali zitachukuliwa kwa watakaobainika kuhusika na tukio hilo.
“Kulingana na aina ya mauaji haya tunaona kabisa si mtu mmoja aliyeweza kufanya tukio hilo hivyo inawezekana ni mtu zaidi ya mmoja kwani wote walikuwa katika vyumba vyao vitatu na miili imekutwa humo katika vyumba hivyo walipokuwa wamelala watu hao,”amesema kaimu Kamanda Sindano.