Jaji Chande: Baadhi ya picha hazikuwa halisi
Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, Jaji Mkuu MstaafuMohamed Chande Othman akisoma Muhtasari wa Ripoti ya Tume hiyo, Ikulu Jijini Dar es Salaam Aprili 23, 2026.
Muktasari:
- Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Vurugu za Uvunjifu wa Amani ya Oktoba 29, 2025 imewasilisha ripoti yake, Mwenyekiti wake Jaji Mohamed Chande, akitaja kilichokutwa na Tume.
Dar es Salaam. Wakati jamii ikiendelea kuwa na maswali mengi kuhusu video ambazo zimekuwa zikisambaa mitandaoni kuhusu kilichotokea katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani katika uchaguzi huo, imesema kulikuwa na picha za kweli na za upotoshaji.
Akiwasilisha ripoti ya Tume hiyo kwa Rais Samia Suluhu Hassan, Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Mstaafu Mohamed Chande amesema baadhi ya picha na video hizo zilikuwa za kweli na zingine zilikuwa zimetengenezwa.
“Uchunguzi umebaini kuwa baadhi ya picha zilizosambaa zilikuwa za kweli na zingine hazikuwa za kweli,” amesema Jaji Chande.
Uchunguzi huu unajibu kiu ya wananchi iliyokuwa ikiendeleza mijadala katika jamii kuhusu ukweli juu ya video na picha nyingi zilizosambaa na kuzua taharuki kutokana na taarifa za kutisha zilizolkuwa zikibeba zikiwemo kuonesha miili ya watu wakiwa wamehifadhiwa hospitalini na vyumba vya maiti.
Katika maelezo yake, Jaji Chande amesema baadhi ya video zilizosambazwa zaidi katika mitandao ya kijamii ni zile zilizotengenezwa akitolea mfano picha iliyosambazwa zaidi ikionesha miili ya watu kwenye mifuko ya bluu.