Maelfu wafurika Uwanja wa Jamhuri kumuaga Magufuli
Muktasari:
- Idadi kubwa ya watu kutoka Dodoma, mikoa ya jirani na nje ya nchi wamefika katika Uwanja wa Jamhuri jijini humo kuaga mwili wa Hayati Rais John Magufuli.
Dodoma. Idadi kubwa ya watu kutoka Dodoma, mikoa ya jirani na nje ya nchi wamefika katika Uwanja wa Jamhuri jijini humo kuaga mwili wa Hayati Rais John Magufuli.
Wakazi hao walioanza kuingia uwanjani saa 12.00 asubuhi wamesema walifika kuanzia saa 11 alfajiri kuwahi kuingia ndani ya uwanja.
Angel Josam ambaye amesafiri kutokea mkoani Singida akibainisha kuwa ameingia uwanjani hapo saa 11:03 alfajiri, “niliona nikichelewa kifika naweza kukosa nafasi ndani ya uwanja, nikaona niwahi, sikutaka kukaa nje ya uwanja, nataka nimuage mpendwa wetu ndani ya uwanja ndio maana nimewahi.”
"Nimetokea mkoani Singida kuja Dodoma ili kumuaga Rais Magufuli, licha ya kuwa nimeona na kusikia taarifa za kifo chake lakini nahisi kama bado tupo naye, sasa nimekuja nishuhudie mwenye.”
Mkazi mwingine Geofrey Sifuni amesema amewasili uwanjani saa 12.34 akitokea wilayani Chamwino mkoani Dodoma.
Amesema kifo cha Magufuli ni pigo kwa Taifa na mtu mmoja mmoja.