Mbaroni akidaiwa kusafirisha mirungi katika gari la kubeba maiti

New Content Item (1)
New Content Item (1)

Muktasari:

Jeshi la Polisi mkoani Tanga limekamata kilo 133 za mirungi iliyokuwa ikisafirishwa katika gari la kubeba maiti lililokuwa likitoka mjini humo kwenda Dar es Salaam.

Handeni. Jeshi la Polisi mkoani Tanga limekamata kilo 133 za mirungi iliyokuwa ikisafirishwa katika gari la kubeba maiti lililokuwa likitoka mjini humo kwenda Dar es Salaam.

Mirungi hiyo iliyokuwa imefungwa kwenye mabunda 1,685 ilikuwa imehifadhiwa kwenye jokofu la kuhifadhia maiti lililopo katika gari hilo.

Akizungumza leo Jumatano Januari 13, 2021 kamanda wa polisi mkoani humo, Blasius Chatanda amesema gari hilo lilikamatwa katika kizuizi cha Polisi kilichopo barabara kuu ya Segera-Chalinze katika kijiji cha Manga kata ya Mkata Wilaya. ya Handeni mkoani Tanga.

Amesema gari hilo aina ya Volvo la kampuni ya Nuru Funeral Service lilikuwa likiendeshwa na Simon Tarimo (37).

Amesema dereva huyo anashikiliwa na polisi na kwamba alikuwa akirejea Dar es Salaam baada ya kupeleka mwili Wilaya ya Same Mkoa wa Kilimanjaro kwa mazishi.

"Dereva huyu aliweka mirungi kwenye mifuko sita zikiwa katika mabunda 1,685 sawa na kilo 133. Alizifunga kwenye jokofu linalotumika kuhifadhia maiti akidhani hatutamgundua" amesema Chatanda.