Mke aomba talaka akidai mumewe kamnyima tendo la ndoa kwa miaka mitano

Mke aomba talaka akidai mumewe kamnyima tendo la ndoa kwa miaka mitano

Muktasari:

  • Adela Ngogolo (42) amefungua kesi ya madai mahakama ya mwanzo Ilala akiomba kupewa talaka na mumewe, Alcado Mkondola (62) kwa madai kuwa ameshindwa kumpatiwa haki yake ya tendo la ndoa kwa miaka mitano mfululizo.

Dar es Salaam. Adela Ngogolo (42) amefungua kesi ya madai mahakama ya mwanzo Ilala akiomba kupewa talaka na mumewe, Alcado Mkondola (62) kwa madai kuwa ameshindwa kumpatiwa haki yake ya tendo la ndoa kwa miaka mitano mfululizo.

Mwanamke huyo anayeishi na mumewe Tabata Kimanga jijini Dar es Salaam ameieleza mahakama hiyo leo Jumanne Aprili  6, 2021 kuwa Mkondola hataki kushiriki tendo la ndoa kwa muda wa miaka mitano na kila akijaribu kumuomba unyumba anasukumwa na kuambiwa akalale chumba cha watoto.

Kesi hiyo ya madai namba 6/2021 aliifunguliwa mahakamani hapo Februari  25, 2021 na inasikilizwa hakimu mkazi wa mahakama hiyo, Benjamin Mwakasonda.

Mwanamke huyo amedai mahakamani hapo kuwa kutoshiriki tendo hilo kwa muda mrefu kumesababisha apate madhara mbalimbali ikiwemo kuugua fangasi sehemu za siri kutokana na kujiingizia vitu visivyofaa ili kutuliza hamu.

Mbali na kuomba talaka, ameomba mahakama ielekeze wagawane mali zote walizochuma na mume wake katika  kipindi chote cha miaka 12 ya ndoa yao.

Akitoa ushahidi wake mahakamani hapo, Adela amedai  Novemba 21, 2009 walifunga ndoa na Mkondola katika kanisa Katoliki Makuburi na maisha yao yalikuwa ya furaha.

Amedai kuwa Padri Peter Thomas wa kanisa hilo ndio aliyewafungisha ndoa yao na kwamba baada ya kufikisha miaka saba ya ndoa, mume wake alianza kubadilika tabia.

"Mume wangu alisafiri kikazi kwenda nchini India wakati huo akiwa mfanyakazi wa shirika la reli na baada ya kurudi kutoka huko alibadilika kitabia ikiwemo kukataa kushiriki tendo la ndoa na mimi nilipokuwa nikimhitaji alinisukuma na wakati mwingine aliniambia nikalale chumba cha watoto," amedai Adela.


Amedai kitendo cha kutokufanya mapenzi kwa miaka mitano mfululizo kimemuathiri kisaikolojia ikiwemo kupata fangasi sehemu za siri.


"Hivyo nikiwa hamu ya kushiriki tendo la ndoa natumia ndizi kumaliza haja zangu, mheshimiwa hakimu nateseka sana na mimi siwezi kutoka nje ya ndoa yangu," amedai.