Mnigeria akaribia kuweka historia WTO

Mnigeria akaribia kuweka historia WTO

Muktasari:

Ngozi Okonjo-Iweala, ambaye amewahi kuwa waziri wa mambo ya nje mara mbili, ameelezewa kuwa ni mtu anayekuwa wa kwanza kufanya mambo.

Abuja, Nigeria (AFP). Ngozi Okonjo-Iweala, ambaye amewahi kuwa waziri wa mambo ya nje mara mbili, ameelezewa kuwa ni mtu anayekuwa wa kwanza kufanya mambo.

Hivi sasa, mwanasiasa huyo mwenye miaka 66 anatarajiwa kuweka tena historia wakati huu akisubiri kuwa Mwafrika na mwanamke wa kwanza kuongoza Shirika la Biashara Duniani (WTO).  

Mbali na muda wake katika ofisi za umma, mchumi huyo wa maendeleo alifanya kazi Benki ya Dunia kwa takriban miaka 25 -- akipanda wadhifa hadi kuwa mkurugenzi mkuu na akishikilia nafasi kubwa mwaka 2012.

"Nadhani ameonyesha uwezo, iwe nchini Nigeria au katika nchi nyingine alizofanya kazi," Idayat Hassan wa Kituo cha Utafiti wa Demokrasia na Maendeleo alisema alipozungumza na AFP.

Akiwa amezaliwa mwaka 1954 mjini Ogwashi Ukwu, katika jimbo la Delta magharibi mwa Nigeria, baba yake ni kiongozi wa kimila. Alitumia muda mwingi wa maisha yake nchini Marekani, akihitimu Taasisi ya Teknolojia ya Massachusetts (MIT) na Harvard, ambako alituma watoto wake wanne.

"Si tu anapendwa nchini Nigeria, anapendwa, kwa sababu ni alama na watu wanamfuatilia kwa sababu ya kile anachofanya kwa wanawake," alisema Hassan.


'Alikaa kimya'

Si kila mmoja anakubali kwamba rekodi yake ni safi.

"Okonjo-Iweala anaweza kuwa amefanya mageuzi ya uwazi katika wizara yake, lakini ukweli ni kwamba takriban mabilioni ya dola kwa mwezi yalikuwa yanapotea katika mapato ya mafuta wakati akiwa waziri wa fedha," alisema Sarah Chayes, mwandishi wa kitabu cha Thieves of State (wezi wa Serikali), kinachohusu rushwa.

"Nadhani ni aibu kwamba anafikiriwa hata kupewa jukumu hilo," alisema Chayes.

"Kuna hamu ya aina hii ya habari nzuri wakati masuala ya makundi ya watu yanapokuwa makubwa, kuwa mwanamke na mweusi haiumi."

Waziri huyo wa zamani amejitanabaisha kama mpambanaji wa rushwa na anasema mama yake alitekwa kutokana na jaribio la kupambana na ufisadi. 

Lakini wakosoaji wanasema angeweza kufanya zaidi kuizuia rushwa wakati akiwa madarakani.

"Angalau alipata nafasi ya kujiuzulu na kuanika rushwa," alisema Olanrewaju Suraju, kutoka kundi la kampeni ya masuala ya maendeleo ya mazingira.

"Badala yake, alikaa kimya na kuruhusu rushwa kutamalaki chini ya utawala wake, na akalalamika baada ya kuondoka ofisini."