Nyani wageuka kero Rombo

Waziri wa maliasili na utalii,Dk.Damas Ndumbaro  akizungumza na wananchi wa kata ya Katangara Mrere wilayani Rombo (hawako Pichani )kuhusu changamoto ya uwepo wa ongezeko la nyani kwenye makazi ya watu.Picha na Janeth Joseph

Muktasari:

  • Madiwani Rombo pamoja wamemwomba Waziri wa maliasili na utalii, DkDamas Ndumbaro kuangalia namna ya kuondoa nyani Wilayani humo ambao wamekuwa tishio kubwa kwa kuwajeruhi watoto wadogo pamoja na kuharibu mazao.

Rombo. Madiwani Rombo pamoja wamemwomba Waziri wa maliasili na utalii, Dk Damas Ndumbaro kuangalia namna ya kuondoa nyani Wilayani humo ambao wamekuwa ni  tishio kubwa kwa kuwajeruhi watoto wadogo pamoja na kuharibu mazao.


Nyani hao wadaiwa kuwa ni wengi  kwenye makazi ya watu ambao hutembea makundi kwa makundi kati ya 40 na 100.
Wametoa ombi hilo wakati Waziri huyo alipofika wilayani humo akiongozana na Naibu wake, Waziri wa Kilimo(mbunge), Katibu mkuu pamoja na viongozi wengine wa Wizara hiyo.


Akizungumzia changamoto ya nyani hao, diwani wa kata ya Katangara Mrere Venance Mallel amesema watu wamekuwa wakishindwa kufanya shughuli za maendeleo kutokana na uharibifu unaofanywa na nyani hao.


"Nyani wamekuwa wengi kuliko hata wakazi wa maeneo haya, wamekuwa wakija kwenye makazi ya watu makundi Kati ya 40 hadi 100,tunaomba kama kuna uwezekano wa kuondoa nyani hawa waondolewe kabisa ,wamekuwa ni waharibifu mno,"alisema Mallel


Diwani wa kata ya Kirongo Samanga, Prisila Yusti amesema watu wamekuwa na hofu kubwa juu ya tishio la nyani hao ambao wamekuwa wakibeba watoto wadogo na kuwajeruhi.


"Tumeteseka sana na hawa nyani ,wamekuwa ni waharibifu kwa kiasi kikubwa sana tunaomba waondolewe maana wamekuwa wakibeba watoto na kuharibu mazao ,tunasumbuka nao sana,"amesema Prisila.


Naye mbunge wa Jimbo hilo ambaye pia ni Waziri wa Kilimo, Profesa Adolf Mkenda amesema zipo jitihada kubwa ambazo zimefanywa na Mamlaka ya Hifadhi za Kilimanjaro (Kinapa) na Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) lakini kero hiyo bado haijaisha na hivyo akamwomba Waziri Ndumbaro kuangalia namna ya kuwahamisha nyani hao kwenye makazi ya watu.


"Sina shukran za kuweza kutosha kuwapa Tanapa na Kinapa kwa jitihada ambazo zilikuwa zikifanywa huko nyuma kwa ajili ya kuwaondoa hawa nyani lakini kero bado haijaondoka , wameendelea kuwa wengi na tishio kwa watu najua hili litapatiwa ufumbuzi na Waziri wetu wa maliasili na utalii ,"amesema Profesa Mkenda