RC Hapi afunga mgodi Bunda

Muktasari:

  • Mkuu wa Mkoa wa Mara Ally Hapi amefunga mgodi wa dhahabu wa Kunanga uliopo wilayani na ameagiza kukamatwa kwa watu wote wanaohusika na uvunjaji wa sheria ikiwa ni pamoja na kuzuia maofisa wa serikali kutekeleza majukumu yao.

Bunda. Mkuu wa Mkoa wa Mara, Ally Hapi amesitisha shughuli uchimbaji katika mgodi wa dhahabu wa Kunanga uliopo wilayani Bunda kwa madai ya kuwepo kwa vitendo vinavyokiuka utawala wa sheria ikiwepo utoroshaji wa madini na uhalifu.

Aidha, Hapi ameagiza kukamatwa kwa watu wote wanaohusika na uvunjaji wa sheria ikiwa ni pamoja na kuzuia maofisa wa serikali kutekeleza majukumu yao.

Kutokana na makosa hayo, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Stoo, Komanya Nzali, Mwenyekiti wa wachimbaji, Peter Marwa na Katibu wa wachimbaji Emanuel Gabriel wamekamatwa na Jeshi la Polisi.

Hapi ametoa maagizo hayo leo Ijumaa Mei 13, 2022 katika eneo la mgodi huo baada ya kufanya mkutano wa hadhara ambapo pamoja na mambo mengine amemuagiza Ofisa Madini Mkazi wa mkoa wa mkazi kufika kwenye mgodi ili kujua hali ya usalama wa mgodi huo.

Hapi amefanya uamuzi huo baada ya kupokea taarifa kutika kwa Ofisa Madini Mkazi wa mkoa wa Mara, Joseph Kumburu kutoa taarifa juu ya mgodi huo ambapo amesema kuwa shughuli za mgodi huo zinafanywa kinyume cha sheria na taratibu.

Kumburu amedai kuwa miongoni mwa changamoto zilizopo mgodini hapo ni pamoja na viongozi wa mgodi  kwa kushirikiana na uongozi wa serikali ya mtaa kukataa kufuata maelekezo wanayopewa juu ya namna ya uendeshaji wa mgodi kwa mujibu wa sheria ya madini.

"Tulikuja hapa Mei 10 kwaajili ya ukaguzi kama sheria inavyotutaka lakini badala yake mwenyekiti wa mgodi kwa kushirikiana na mwenyekiti wa mtaa na wengine walituzuia kufanya kazi ikafika hatua wakamjeruhi askari na kuanza kurusha mawe kutaka kutujeruhi," amesema Kumburu.

 Amesema kuwa mgodi huo pia sio salama kwa wachimbaji, kwani kumekuwepo na matukio ya vifo vya wachimbaji wadogo, akitoa mfano wa vifo vya wachimbaji watatu vilivyotokea hivi karibuni.

Amesema kuwa Aprili 20 mwaka huu alizuia uongozi wa mgodi kugawa mifuko ya mawe kabla ya kupewa utaratibu ikiwemo namna ya kutoa kodi ya serikali lakini uongozi wa mgodi ulikaidi na kugawa mawe hayo hali iliyoplekea serikali kukosa mapato.

"Hapa kuna utoroshaji wa madini na hata kule kwenye soko letu huwezi kuwasoma kwenye mtandao na hii inafanywa na viongozi wakiwemo wa serikali, vyama vya siasa na wachimbaji" amesema Kumburu.

Kufuatia hali hiyo Hapi amesema kuwa serikali ya mkoa wa Mara haitavumilia mtu yoyote anayekiuka sheria na taratibu na kwamba huo sio utawala wa sheria


" Kwa yanayoendela hapa ina maana kuna utawala umetengenezwa ndani ya utawala mwingine hii haikubaliki nafunga huu mgodi pia nikuagize afisa madini ndani ya wiki moja kutana na wenye mashamba na wenye leseni kutengeneza mazingira ya kazi salama" amesema

Awali Mwenyekiti wa wachimbaji, Peter Marwa alisema kuwa kuna wawekezaji waliopewa leseni kwajaili ya kufanya shughuli za uchimbaji katika eneo hilo ambao alidai kuwa ndio chanzo cha mgogoro mgodini hapo.

" Kuna huyo anaitwa JB and partners hawa historia inaonyesha kuwa kila mgodi waliofanya kazi lazima kuna mgogoro na sisi hapa hatuwataki tuna uwezo wa kumiliki  leseni tunaomba wafutiwe umiliki ili wenye mashamba hapa wamilikishwe leseni" amesema Marwa