Saratani kwa watoto wa kiume yatikisa KCMC
Muktasari:
- Daktari bingwa wa magonjwa ya damu na saratani kwa watoto hospitali ya rufaa ya Kanda ya Kaskazini (KCMC), Dk Esther Majaliwa amesema asilimia 57 ya watoto wanaokutwa na saratani ya mfumo wa damu na tezi ni wa kiume ikilinganishwa na asilimia 43 ya watoto wa kike wanaobainika kuwa na ugonjwa huo.
Moshi. Daktari bingwa wa magonjwa ya damu na saratani kwa watoto hospitali ya rufaa ya Kanda ya Kaskazini (KCMC), Dk Esther Majaliwa amesema asilimia 57 ya watoto wanaokutwa na saratani ya mfumo wa damu na tezi ni wa kiume ikilinganishwa na asilimia 43 ya watoto wa kike wanaobainika kuwa na ugonjwa huo.
Amesema wagonjwa wapya 298 ambao ni sawa na asilimia 15.5 waligundulika kwa mara ya kwanza katika hospitali hiyo kuwa na ugonjwa wa saratani ambapo asilimia 54 ni watoto wenye umri chini ya miaka 10.
Ameeleza hayo jana Ijumaa Septemba 10, 2021 katika maadhimisho ya mwezi wa saratani kwa watoto ambayo kila mwaka hufanyika katika hospitali hiyo.
Katika maadhimisho hayo yaliyokwenda sambamba na matembezi ya zaidi ya kilomita tatu Dk Majaliwa amesema, "tunapata watoto wengi sana wa kiume hapa wenye saratani, bado hatujajua ni kwa nini lakini kuna utafiti tunahitaji kufanya kujua sababu watoto wengi ni wa kiume."
“Tukiangalia kutoka mwaka 2016 hadi 2021 hospitali hii ilitibu watoto 2000 wenye saratani na kati ya hao 298 ni wapya ambao ni sawa na asilimia 15.5. Asilimia 43.2 ya saratani tunazozibaini ni za mfumo wa damu na tezi na idadi ya wagonjwa inaongezeka."
"Kikubwa ambacho jamii inapaswa kujikinga na ugonjwa huu hasa kwa watoto wadogo ni chanjo, hizi chanjo ambazo wanapata utotoni zinasaidia kuzuia virusi na magonjwa mbalimbali ambayo yanaweza kumletea mtoto hali ya kupata saratani,” amesema Dk Majaliwa.
Mkurugenzi mtendaji wa hospitali hiyo, Profesa Gileard Masenga ameishukuru Serikali kwa kutenga Sh4 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa jengo maalum la tiba ya mionzi katika hospitali hiyo na kwa mwaka inapokea wagonjwa 5000 hadi 6000.