Serikali kuboresha maeneo ya makumbusho

Arusha. Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja amesema kiasi cha Sh2.2  bilioni za  Uviko-19 zilizotolewa kwa ajili ya kuboresha Makumbusho ya Malikale zimeendelea kuboresha kwa kiasi kikubwa.


Ameyasema hayo leo Machi 16  jijini Arusha wakati  Kamati ya  Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii ilipotembelea miradi ya Uviko-19 katika makumbusho ya Azimio la Arusha na elimu viumbe na kueleza endapo Malikale zitaendelea kuboreshwa zinaweza kuutangaza utalii wa nchi kwa kiwango cha juu.

Aidha Masanja amesema kuwa bado maboresho yanahitajika zaidi ili kuweza kuweka historia vizuri ya uhifadhi kwa njia ya Malikale kupitia majumba ya makumbusho yaliyopo nchini.


Amesema makumbusho zinaendeshwa kwa kusuasua kutokana na ufinyu wa bajeti  ambapo kwa sasa hivi wamejipanga kuweka kipaumbele katika maboresho mbalimbali ili kuhakikisha makumbusho hayo yanavutia na kuleta watalii wengi zaidi.


"Serikali imejiwekea mikakati mbalimbali ya kuhakikisha maeneo yote yaliyosahaulika yanaboreshwa zaidi  ili yakawe na maonekano  wa kisasa ili kuweza kuongeza  mapato  na idadi ya watalii wanaotembelea maeneo hayo." amesema


Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi makumbusho ya Taifa, Dk Oswald Masebo amemshukuru  Rais Samia kwa kuwekeza katika sekta hiyo na wamepokea maelekezo na mapendekezo na watayafanyia  kazi kwa ajili ya kujipanga wenyewe na kuzifanyia mazoezi makubwa.


Aidha ameomba kamati hiyo kuongeza bajeti ya kutosha kwa ajili ya shirika ili  kuweza kuboresha zaidi miundombinu mbalimbali na kufanya marekebisho makubwa .


Kwa upande wake Mkurugenzi wa makumbusho ya maazimio la Arusha, Dk Gwakisa Kamatula amesema kiasi cha Sh 112 milioni kilitengwa kwa ajili ya maboresho na ukarabati wa  wa Azimio  la Arusha ambapo kwa sasa hivi  mradi umekamilika kwa asilimia 100.


Mkurugenzi wa Makumbusho ya elimu viumbe Arusha, Christina Ngereza amesema kiasi cha Sh272 milioni zilitolewa na serikali kwenye Uviko kwa ajili ya miradi minne ya makumbusho ya elimu viumbe  Arusha .


Ngereza amesema miradi hiyo ni onesho la Tembo na wanyama watano  wakubwa onesho la wanyama aina ya Reptilia, uboreshaji wa maabara ya bailojia na uboreshaji  wa stoo ya bailojia.