Serikali kupitsha fedha zake KCBL ili kuimarisha
Muktasari:
- Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amesema Serikali imeridhia kupitisha fedha zote za maendeleo ya mkoa huo kwenye benki ya ushirika ya KCBL ili kuiimarisha kutokana na changamoto ya mtaji ulioikumba.
Moshi. Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amesema Serikali imeridhia kupitisha fedha zote za maendeleo ya mkoa huo kwenye benki ya ushirika ya KCBL ili kuiimarisha kutokana na changamoto ya mtaji ulioikumba.
Mghwira amesema fedha hizo ni pamoja na mapato ya ndani ya Halmashauri zote 7 za mkoa huo ambapo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuiimarisha na kuinyanyua benki hiyo.
Ameyasemwa leo Februari 8 mjini Moshi wakati wa hafla fupi ya kuwaaga waliokuwa wajumbe wa bodi ya mpito ya benki hiyo ambayo imedumu kwa miaka miwili.
“Tumeiomba Serikali kwamba tupitishie fedha za maendeleo katika benki hii ambapo ni pamoja na fedha za mapato yetu ya ndani ambapo tayari tumeshakubaliwa.
“Halmashauri zetu sasa zinaweza kununua hisa kwa njia hiyo na wakawa na hisa kwenye benki hii ambapo itaziletea faida ,” alisema Mghwira
"Mpaka sasa tumefanya kazi kubwa sana kurudisha benkii hii sokoni na tayari watu wameshaanza kuja kwa wingi lakini sasahivi tunahitaji kukuza mtaji hadi kufikia sh.100 bilioni za kuanzia ," alisema
Amesema awali walikuwa wakitafuta wawekezaji wakubwa ambao wangeweza kununua asilimia 20 ya hisa na tayari benki ya CRDB ilionyesha nia na kutoa kiasi cha Sh1.5 bilioni kilichosaidia benki hiyo kufika hapo.
Kwa upande wake Meneja wa benki hiyo, Godfrey Ng’ura amesema kwa sasa wamerejesha huduma zote kama kawaida tangu mwaka jana.
“Katika miezi mitatu tumefungua zaidi ya akaunti mpya 200 zenye thamani ya sh.600 milioni na tumeendelea kutoa mikopo takribani Sh700 milioni pamoja na huduma na bidhaa mbalimbali ambazo tunaendelea kutoa kwa wateja wetu,” amesema Ng’ura